JE! WENGI WANAWEZA KUKOSEA?

Katika Mwongozo 16 tuligundua kwamba kulionja pumziko la Sabato ni tiba muhimu kwa maisha ya siku hizi yaliyojaa msongo mwingi. Kwa kuwa Mungu anaelewa kila haja tuliyonayo , aliiweka kila siku ya saba kwa ajili ya pumziko letu la kimwili na burudiko letu la kiroho. Baada ya kuiumba dunia yetu kwa siku sita, yeye "akapumzika" katika siku ile ya saba, "akaibariki" na "kuifanya takatifu" (mwanzo 2:1-3).

Mungu alipowapa watu wake Amri kumi, yaani, wana wa Israeli, aliiweka amri ya kuitunza Sabato ya siku ya saba katikati ya sheria yake (Amri kumi) (Kutoka 20:8-11). Kulingana na amri hiyo, Sabato ni ukumbusho wa uweza wa Mungu wa Uumbaji, ni siku ya kutulia na kutafakari juu ya uzuri na maajabu ya kazi zake alizoziumba, ni siku ya kustarehe na kumkaribisha sana Muumbaji wetu, siku ya kuchunguza kwa kina zaidi uhusiano wetu na yeye.

Katika kipindi kile cha maisha ya kibinadamu ya Yesu aliyoishi hapa duniani, yeye pia aliitunza Sabato (Luka 4:16) na kuiidhinisha kama siku inayowaletea Wakristo manufaa (Marko 2:27,28.) Mafungu kadhaa katika kitabu cha Matendo yanaonyesha wazi kwamba wanafunzi wake Kristo waliabudu katika siku ya Sabato baada ya ufufuo wake (Matendo 13:14, 16:13, 17:2, 18: 1-4, 11).

1. Suala Lenye Utata

Hiyo inatufikisha sisi kwenye somo ambalo wengi huliona kuwa lina utata kwao. Kwa kipindi fulani ulimwengu wa Kikristo umekuwa ukizitunza siku mbili tofauti. Kwa upande mmoja, Wakristo wengi sana kwa unyofu wa moyo wanaitunza Jumapili, siku ya kwanza ya juma, ambayo wao wanaamini kwamba ndiyo ukumbusho wa ufufuo wake Kristo. Kwa upande ule mwingine, kundi kubwa la Wakristo, nao vilevile wakiwa ni wanyofu wa moyo, wanaamini kwamba Biblia inaipa heshima siku ya saba peke yake kama ndiyo Sabato na ya kwamba hakuna mahali popote inapothibitisha utakatifu wa Jumapili.

Je! inaleta tofauti yeyote juu ya siku gani tunayoitunza kama Sabato? Sisi kama watu walio wanyoofu wa moyo na wenye ari tunaotaka kuijua kweli, ni lazima tujiulize wenyewe swali hili. "Je! Ni jambo gani ambalo ni maana kwa Yesu? Hivi Yesu anataka mimi nifanye nini?

Katika kufikiria uamuzi wa jambo hilo, mambo kadhaa ya maana hayana budi kuwekwa wazi, je ni nani aliyeibadili Sabato kutoka Jumamosi siku ya saba ya juma, kwenda Jumapili siku ya kwanzia ya juma? Je! Hivi Biblia inatoa idhini kwa badiliko kama hilo?Kama jibu ni ndiyo, Je, Mungu, Kristo, au labda wale mitume ndio waliofanya badiliko hilo?

Tutaendelea mbele kwa kuangalia uwezekano wo wote uliopo

2. Je! Ni Mungu Aliyebadili Siku?

Je! Kuna tamko lolote toka kwa Mungu ambalo linaibadilisha Sabato kutoka siku ya saba kwenda siku ya kwanza ya juma?

Wakristo wengi sana wanazikubali Amri kumi kama mwongozo halali ambao kwa huo sisi tunpaswa kuishi. Huu ni ujumbe wa pekee ambao Mungu mwenyewe amepata kuandika kwa ajili ya wanadamu. Ni za muhimu sana, aliziandika juu ya mbao za mawe kwa kidole chake mwenyewe (Kutoka 31:18).

Katika ile amri ya nne Mungu anatuagiza sisi anasema:
"Ikumbeke siku ya Sabato uitakase. Siku sita fanya kazi na kutenda mambo yako yote, lakini SIKU YA SABA NI SABATO YA BWANA, MUNGU WAKO. Siku hiyo usifanye kazi yoyote, … maana kwa siku siku sita BWANA alifanya mbingu, na nchi, na bahari na vyote vilivyomo, lakini AKAPUMZKA siku ya saba. Kwa hiyo BWANA AKAIBARIKI siku ya Sabato AKAITAKASA" - Kutoka 20:8-11.

Mungu alipowapa watu wake zile Amri kumi, pia alieleza wazi kwamba maagizo yale yaliyotoka kinywani mwake asiwepo mwanadamu yeyote wa kuyafanyia marekebisho yeyote ili kuyafanya yawe bora zaidi au kuondoa maneno yake yeyote anapofanya uhariri wake.

"MSIONGEZE neno lolote katika yale niwaamuruyo, wala MSIPUNGUZE neno lolote, bali zishikeni amri (kumi) za BWANA, Mungu wenu ninazowapa ninyi" - (Kumbukumbu la Torati 4:2).

Mungu mwenyewe anatoa ahadi kwamba hawezi kuzibadili amri zake [kumi]:
"MIMI SITALIVUNJA agano langu, wala SITABADILI NENO LILILOTOKA MIDOMONI (MWANGU) - (Zaburi 89:34).

Biblia inaeleza waziwazi kwamba Mungu hakubadili Sabato kutoka siku ya saba kwenda ile ya kwanza ya juma.

3. Je! Yesu Aliibadili Sabato?

Kulingana na maneno ya Yesu, Amri kumi haziwezi kubadilika kamwe:
"Msidhani ya kuwa nimekuja kutangua sheria na mafundisho ya manabii. Sikuja kutangua bali kukamilisha. Kweli nawaambieni, mpaka hapo mbingu na dunia zitakapopita, hakuna hata nukta moja au sehemu ndogo kabisa ya sheria itakayoondoka mpaka yote yametimia" - (Mathayo 5:17-18).

Katika Mwongozo 16 tuligundua kwamba desturi ya Yesu ilikuwa ni kwenda kuabudu katika sinagogi siku ya Sabato (Luka 4:16). Pia tuligundua kwamba Yesu alitaka wanafunzi wake waendelee kuionja raha ya kuitunza ile Sabato ya kweli (Mathayo 24:20)

Ni dhahiri, basi, kwamba kutokana na mafundisho ya Yesu na kielelezo chake sisi bado tunayo haja ya hilo pumziko la Sabato, yaani, kustarehe na kuutumia wakati wetu pamoja na Mungu.

4. Je! Wale Mitume Waliibadili Sabato?

Yakobo, kiongozi wa kwanza wa kanisa lile la mwanzo, aliandika maneno haya kuhusu zile Amri kumi:
"Anayevunja amri mojawapo ya sheria, atakuwa na hatia ya kuivunja sheria yote. Maana yule yule aliyesema: "USIZINI, "alisema pia" "USIUE." Kwa hiyo, hata ikiwa hukuzini, lakini umeua, wewe umeivunja sheria" - (Yakobo 2:10, 11).

Luka, tabibu na mwinjilisti katika kanisa lile la kwanza, anatoa taarifa hii.

"Siku ya Sabato tukatoka nje ya mji, tukaenda kando ya mto, ambapo tulidhani kuwa mahali pa kusali. Tuliketi, tukiongea na wanawake waliokusanyika mahali hapo" - (Matendo 16:13).

Kitabu cha Matendo cha Agano Jipya kinataja mara 84 ilipotunzwa. Sabato hiyo na wafuasi wa Kristo, zote hizo zilikuwa zikitunzwa zaidi ya miaka 14 baada ya ufufuo wa Yesu: Sabato 2 pale Antiokia (Matendo 13:14,42,44); 1 pale Filipi (Matendo 16:13), 3 pale Thesalonike (Matendo 17:2,3), Sabato 78 pale Korintho (Matendo 18:4,11).

Yohana, wa mwisho kufa miongoni mwa wale mitume kumi na wawili, aliitunza Sabato. Aliandika hivi:
"Siku ya Bwana nilikuwa katika Roho" - (Ufunuo 1:10).

Kulingana na maneno ya Yesu, siku ya Bwana ni Sabato:
"Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa Sabato" - (Mathayo 12:8).

Uchunguzi wa ushahidi wa maandiko unaoonyesha wazi kwamba wale mitume hawakufanya jaribio lolote la kuibadili siku ya Mungu ya mapumziko kutoka siku ya saba kwenda ile siku ya kwanza ya juma. Agano jipya, linaitaja siku hiyo ya kwanza ya juma mara nane tu. Katika mifano hiyo yote hakuna ambapo siku ya kwanza ya juma inatajwa kuwa ni takatifu, wala hata kudokezwa kuwa tunapaswa kuitenga kama siku ya ibada. Uchunguzi uliofanywa kwa makini sana wa hayo mafungu manane yanayoitaja siku ya kwanza ya juma huonyesha matukio haya yaliyotokea Jumapili:

(1) Wanawake walikwenda kaburini siku ile ya kwanza ya juma (Mathayo 28:1).
(2) "Hata Sabato ilipokwisha" wanawake wakaanza tena kufanya shughuli zao za kidunia katika siku ile ya kwanza ya juma (Marko 16:1,2).
(3) Yesu alimtokea kwanza Mariamu Magdalena mapema siku ile kwanza ya juma (Marko 16:9).
(4) Wafuasi wa Yesu walianza tena kufanya shughuli zao katika ile siku ya kwanza juma (Luka 24:1).
(5) Mariamu alikwenda kwenye kaburi lile la Yesu na kulikuta kaburi liko tupu katika ile siku ya kwanza (Yohana 20:1).
(6) Wanafunzi wale walikusanyika mahali pamoja "kwa hofu ya Wayahudi" (si kwa ajili ya kuendesha ibada ) Katika ile siku ya kwanza ya juma (Yohana 20:19).
(7) Paulo aliwaomba washiriki wa kanisa kufanya mahesabu ya fedha zao walizopata katika ile siku ya kwanza ya juma, na "kuweka kando kiasi fulani cha fedha" kwa ajili ya maskini kule Yerusalemu (I Wakorintho 16:1,2). Kifungu hicho hakitaji mkutano wowote wa dini ambao ulifanyika.
(8) Katika Matendo 20:7 Luka anaongea habari za hotuba (mahubiri) ya Paulo aliyoitoa katika ile siku ya kwanza ya juma wakati wa mkutano ule wa kuagana ambao haukutazamiwa kufanyika. Kusema kweli, Paulo alihubiri kila siku, na mitume wale walimega mkate kila siku (Matendo 2:46).

Hakuna hata moja kati ya mafungu hayo linalodokeza ya kwamba wale mitume waliazimu kuacha kuitunza Sabato ya siku ya saba. Mitume wale hawakulitaja badiliko lolote la Sabato kutoka siku ya saba kwenda ile ya
kwanza ya juma. Hakuna ushahidi wowote ulio wazi katika Agano Jipya unaoonyesha badiliko hilo la Sabato kutoka Jumamosi, siku ya saba ya juma, kwenda Jumapili, siku ya kwanza ya juma. Badiliko hilo lilikuja baada ya siku zile za Yesu na mitume wake, kwa hiyo, yatupasa sisi kuigeukia historia ili kuona ni lini na kwa jinsi gani badiliko hilo lilitokea.

5. Jumapili Ilitoka Wapi?

Mitume wale wanatuonya sisi waziwazi kwamba Wakristo fulani wangetangatanga na kwenda mbali na mafundisho ya Ukristo ule wa Agano Jipya: "Iweni macho " (Matendo 20:29-31). Na ndivyo ilivyotokea hasa. Wanahistoria wanaoaminika wanaandika waziwazi kuonyesha jinsi Wakristo walivyoanza kupotea na kuuacha usafi ambao kanisa lile la mitume lilikuwa nao. Mapokeo na mafundisho ambayo hayakuungwa mkono kamwe na Paulo, Petro na waasisi wale wengine wa kanisa lile la Kristo, yakaanza kuingia taratibu ndani ya kanisa.

Badiliko lililofanyika kutoka katika utunzaji wa Sabato kwenda kwenye utunzaji wa Jumapili lilitokea baada ya kukamilika kuandikwa kwa Maandiko ya Agano jipya na baada ya kufa mitume wale wote. Historia inaandika katika kumbukumbu zake ya kwamba hatimaye Wakritsto wakahama kutoka katika kufanya ibada yao na kupumzika siku ya saba kwenda katika siku ile ya kwanza ya juma. Lakini, kwa kweli, waumini hawakuacha kuitunza Sabato ile ya siku ya saba mwishoni mwa juma fulani lililowekwa na ghafla kuanza kuitunza Jumapili kama siku ya Bwana. Mfano mmoja uliothibitishwa ambao ulitokea mapema sana wa utunzaji wa Jumapili na Wakristo ulitokea katika nchi ya Italia, katikati ya karne ile ya pili baada ya pale Wakristo wengi walizitunza siku zote mbili, ambapo wengine bado waliendelea kuitunza Sabato peke yake.

Tarehe 7 Machi, 321 B.K Konstantino Mkuu alitoa amri ya kwanza ya Kiserikali ya Jumapili, akawalazimisha wote, isipokuwa wakulima, katika Dola ya Kiroma kupumzika Jumapili. Hivyo pamoja na sheria nyingine zipatazo tano za kiserikali zilizoamriwa na Konstantino kuihusu Jumapili, ziliweka mfano wa sheria zote za Jumapili kuanzia wakati ule mpaka leo. Katika ile karne ya nne Baraza la Laodikia liliwakataza Wakristo wasiache kufanya kazi siku ya Sabato, huku likiwashurutisha kuiheshimu Jumapili kwa kuacha kufanya kazi endapo uwezekano ulikuwapo wa kufanya hivyo.

Historia inaonyesha kwamba ibada ya Jumapili na utunzaji wake ni desturi iliyowekwa na wanadamu. Biblia haitoi kibali chochote ili kuifutilia mbali Sabato ya siku saba ya amri ile ya nne. Nabii Danieli alitabiri kwamba katika kipindi kile cha Kikristo mamlaka fulani yenye hila ingejaribu kuibadili sheria ya Mungu (Amri Kumi) (Danieli 7:25)

6. Ni Nani, Aliyefanya Badiliko?

Je! Ni nani aliyeihamisha rasmi Sabato kutoka siku ya saba kwenda siku ya kwanza ya juma? Kanisa Katoliki linadai kwamba limefanya badiliko hilo. Katika jitihada ya kutaka kuiokoa Dola ya Roma iliyokuwa inavunjika, viongozi wa kanisa waliokuwa na kusudi zuri wakafanya maridhiano na kujaribu kubadili siku ya ibada kutoka Jumamosi kwenda Jumapili.

Katekisimo ya kanisa Katoliki la Roma inasomeka hivi:
"Swali: Ipi ndiyo siku ya Sabato?
"Jibu: Jumamosi ndiyo siku ya Sabato.
"Swali: Kwa nini sisi tunaitunza Jumapili badala ya Jumamosi?
"Jibu: Tunaitunza Jumapili badala ya Jumamosi kwa sababu kanisa Katoliki …. Liliihamisha ibada toka Jumamosi kwenda Jumapili".
- Peter Geirmannn, The Convert's Catechism of Catholic Doctrine (toleo la 1957). Uk. 50.

Kwa majivuno kanisa Katoliki linatangaza kwamba viongozi wa kanisa ambao ni wanadamu tu ndio waliofanya badiliko hilo.

"Siku ile takatifu, yaani, Sabato, ilibadilishwa kutoka Jumamosi kwenda Jumapili... si kutokana na maagizo yo yote yaliyoonekana katika Maandiko bali kutokana na hisia ya kanisa kwamba linao uwezo wake lenyewe… watu wale wanaofikiri kwamba Maandiko ndiyo yangekuwa mamlaka peke yake, kwa mantiki hiyo, ingewapasa kuwa Waadventista Wasabato , nao wangeitakasa Jumamosi." - Cardinal Maida, Askofu Mkuu wa Detroit, Saint Catherine Catholic Church Sentine, Algonac, Michigan, Mei 21, 1995.

7. Je! Makanisa Ya Kiprotestanti Yanasemaje?

Hati rasmi zinazotoa muhtasari wa itikadi za madhehebu kadhaa ya Kiprotestanti zinakiri kwamba Biblia haitoi kibali cho chote cha kuitunza Jumapili.

Martin Luther, mwasisi wa kanisa la Kilutheri, aliandika katika ungamo la Augusiburgi (Augusburg Confession), sharti la imani la 28, aya ya 9, maneno haya: "Wao [Wakatoliki wa Roma] wanadai kwamba Sabato ilibadilishwa na kuwa Jumapili, siku ya Bwana, kinyume na ile sheria ya Amri kumi,.. wala hakuna mfano wanaojivunia sana kama huo wa kuibadili siku ya Sabato. Ni mkuu, wasema wao, uwezo na mamlaka ya Kanisa, kwa kuwa liliiondoa mojawapo ya zile Amri kumi."

Wanatheolojia wa Kimethodisti Amosi Binney na Danieli Steele walitoa maoni yao haya:
"Ni kweli, hakuna amani dhahiri ya ubatizo wa watoto wachanga….wala hakuna yo yote ya kuitakasa siku ya kwanza ya juma." Theological Compend (New York: Methodist Book Concern, 1902), Kurasa 180,181.

Dk. N. Summerbell, mwanahistoria wa wanafunzi wa Kristo (Disciples of Christ) au Kanisa la Kikristo (Christian Church), aliandika, alisema:
"Kanisa la Roma lilikuwa limeasi kabisa…..Liliigeuza Amri ya Nne kwa kuiondoa Sabato ile ya Neno la Mungu, na kuiweka Jumapili kama siku takatifu" A True History of the Christian and the Christian Church, kurasa za 417,418.

8. Suala Lenyewe hasa ni lipi?

Jambo hilo linatuleta ana kwa ana kupambana na maswali haya: kwa nini Wakristo wengi sana huitunza Jumapili bila kuwa na idhini ya Biblia? La maana zaidi ni hili, Je! Niitunze siku gani? Je! Niwafuate wale wasemao, "Sidhani kwamba inaleta tofauti yoyote kuhusu siku gani ninayoitunza mradi tu mimi naitunza moja katika zile saba"? Au, Je! Niihesabu kuwa ni ya maana ile siku ambayo Yesu, Muumbaji wetu, aliianzisha alipoiumba Dunia yetu hii, tena ni siku ile aliyoiteua Mungu na kuiweka katika zile Amri kumi: yaani, kwamba "siku ya saba ni Sabato"?

Hapa tunashughulika zaidi ya utunzaji wa nje tu, bali juu ya siku ipi yaonekana kibiblia kuwa ni sahihi. Hoja muhimu inayohusu hapa ni ile ya utii kwa Yesu. Muumbaji wetu aliitenga Sabato kama siku "Takatifu," kama ndio wakati uliowekwa kwa ajili yetu na familia zetu kumkaribia yeye zaidi ili tupate kupewa nguvu na burudiko. Nitamtii nani? Je! Nimtii Kristo, mwana wa Mungu, au mapokeo ya wanadamu katika suala hili la siku ninayoitakasa? Uchaguzi uko wazi: mafundisho ya wanadamu au amri za Mungu. Neno la wanadamu au Neno la Mungu. Siku mbadala iliyowekwa na wanadamu au amri ya Mungu.

Nabii Danieli anatoa onyo kwa wale ambao wange"jaribu kubadili majira yaliyowekwa pamoja na sheria" (Danieli 7:25,NIV) ["azimu kubadili majira na sheria" (Daniel 7:25, NKJV)]. Mungu anawaita watu wake warudi na kumtii yeye. Anawaita ili wapate kuitunza Sabato kama ishara ya Utii na upendo wao kwake yeye.

Yesu alisema, "Mkinipenda, mtakishika kile niwaamurucho" (Yohana 14:15). Tena yeye anaahidi kuwapa furaha kamili wale wampendao hata kuweza kuzitii amri zake (Yohana 15:9-11). Tunaye Mwokozi wa ajabu. Anayo shauku nyingi kwa ajili yetu ili sisi tupate kuuonja upendo wake kwa utimilifu wake wote. Moyo ule ulio na utii wa hiari unafungua mlango wazi ili kuupokea upendo huo.

Katika ile bustani ya Gethsemane Kristo alijinyenyekeza kikamilifu chini ya mapenzi ya Baba yake - licha ya kukabiliwa na msalaba na dhambi za ulimwengu mzima zilizokuwa zikiyaangamiza maisha yake. Alipomlilia Mungu, na kusema, "Uniondolee kikombe hiki," alikuwa amejinyenyekeza katika maombi yake, kisha akaongeza kusema hivi "Walakini, si kama nitakavyo mimi, bali utakavyo wewe" (Marko 14:36).

Kristo anatamani sana kwamba sisi tupate kuuonja utimilifu ule uletwao na maisha yaliyosalimishwa kweli kweli. Pia anataka sisi tuionje furaha ya pumziko la Sabato. Anataka sisi tumtumainie yeye kiasi cha kutosha kumtii katika mambo yote ya maisha yetu. Endapo wewe utaitika anapokuita na kuzitii amri zake zote [kumi], basi, wewe utaweza kuionja ahadi ya Yesu isemayo kwamba furaha yake itakuwa "ndani yenu" na "furaha yenu" ita "timizw[a]" (Yohana 15:11).


© 2004 The Voice of Prophecy Radio Broadcast
Los Angeles, California, U.S.A.