KUINGIA KATIKA MAISHA YA KIKRISTO

Hapa ni barua ya kusisimua sana toka kwa mmojawapo wa wawakilishi wa Shule yetu ya Biblia katika Afrika.

" Miaka mitano iliyopita nilipokea ombi toka kwa sauti ya Unabii ili nimtembelee mfungwa mmoja ambaye alikuwa mwanafunzi wa Shule ya Biblia kwa Posta. Nilionyesha ombi lile kwa wakuu wa gereza lile ambao kwa hisani yao walinipa ruhusa. Kwa kuwa mwanafunzi yule alikuwa na hamu kubwa sana ya kujifunza Biblia, basi, nilimtembelea mara kwa mara.

"Karibu miezi sita baada ya kumtembelea mara ya kwanza, aliomba kubatizwa na kujiunga na kanisa. Wakuu wale walikubali kuandaa mahali ili ubatizo ule ufanyike ndani ya gereza lile. Wasimamizi wao pamoja na wafungwa wengine walikusanyika pale kushuhudia ubatizo ule niliopata kuufanya ambao uliigusa mioyo yao.

"Muda mfupi baada ya tukio lile, ndugu yetu yule alifunguliwa toka kifungoni, ingawa bado alikuwa na muda mrefu wa kutosha kutumikia kifungo chake. Nilipouliza imekuwaje, niliambiwa kwamba maisha yake yalikuwa yamebadilika kabisa, naye akawa shahidi aliyemshuhudia Mwokozi wake, na dini yake hata hakuweza tena kufikiriwa kama mfungwa wala kutendewa kama mfungwa. Mtu yule akaungana na familia yake na sasa ni kiongozi katika mojawapo ya makanisa yenye watu wengi."

1. Ubatizo Maana Yake Nini?

Mfungwa yule alipogeuka na kuwa Mkristo na maisha yake yalipobadilika kabisa, kwa nini ilikuwa ni lazima kwake kubatizwa? Katika mazungumzo yake na Nikodemo, Yesu anaonyesha umuhimu na maana ya huo ubatizo:
"Hakuna mtu ye yote awezaye kuuona ufalme wa Mungu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho" - Yohana 3:3,5.

Basi kulingana na Yesu ni lazima sisi tuzaliwe " kwa maji na kwa Roho." Katika maisha mapya kupitia katika badiliko la mawazo na moyo. Kwa kuwa kuingia katika ufalme wa Mungu kunataka maisha mapya kabisa, si yale maisha ya zamani yaliyotiwa viraka, ndiyo maana yanaitwa kuzaliwa upya. Ubatizo wa maji ni ishara ya nje inayoonyesha badiliko hilo la ndani. Mwakilishi wetu alimbatiza yule mfungwa kama ishara ya kutambua kujitoa kwake kwa Kristo na ishara ya badiliko kamili ambalo Roho Mtakatifu alikuwa ameanza kufanya katika tabia yake.

2. Kwa Nini Mimi Nibatizwe?

Wokovu wetu unayazunguka matendo makuu matatu ya Kristo.

"Kristo ALIKUFA kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo Maandiko, … ALIZIKWA, … ALIFUFUKA siku ya tatu, kama yanenavyo Maandiko" - (1 Wakorintho 15:3,4).

Kristo alifanya wokovu huo uwezekane kwa njia ya kifo chake, kuzikwa kwake, na kufufuka kwake.

"Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu TULIBATIZWA KATIKA MAUTI YAKE? Basi TULIZIKWA PAMOJA NAYE KWA NJIA YA UBATIZO katika mauti yake, kusudi KAMA KRISTO ALIVYOFUFUKA KATIKA WAFU kwa njia ya utukufu wa Baba, VIVYO HIVYO NA SISI TUPATE KUISHI MAISHA MAPYA." - Warumi 6:3,4.

Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, alizikwa, kisha alifufuka katika kaburi ili kutupa sisi maisha mapya ya haki. Kwa kubatizwa sisi tunashiriki kabisa katika kifo, kuzikwa, na kufufuka kwake Yesu. Ubatizo una- maanisha kwamba sisi tumeifia dhambi pamoja na Kristo, kisha tunafufuka na " Kuishi maisha mapya" ndani ya Kristo. Kifo chake Kristo ufufuo wake huwa ni Kifo chetu na ufufuo wetu. Mungu anaweza kutufanya sisi kuwa hai katika mambo yale ya Roho kana kwamba sisi tulikuwa tumefufuliwa katika wafu. Tendo la kimwili la ubatizo kwa picha huwakilisha hatua za kuongoka.

Kwanza, tunaingizwa ndani ya maji, yaani, tunazamishwa majini kabisa, sawasawa tu na watu ambao wamekufa wanavyoshushwa kaburini na kufunikwa na udongo. Hii ni kusema kwamba sisi tunapenda kufa pamoja na Kristo na kuyazika maisha yetu yale ya zamani. Ubatizo ni mazishi (maziko), ni kuyaaga rasmi maisha yale ambayo yalitawaliwa sana na dhambi. Halafu, tunanyanyuliwa juu kutoka ndani ya maji na yule anayebatiza, sawasawa tu na mtu anayefufuliwa kutoka kaburini. Hii ni kusema kwamba sisi ni " [vi]umbe vipya" tumejitoa kabisa kuishi hayo maisha mapya anayotupa Mungu.

Ni kuzamishwa ndani ya maji peke yake kunakoweza kuonyesha kielezo sahihi cha maana halisi ya ubatizo - yaani, kifo, kuzikwa na kuzaliwa upya. "Ubatizo" kwa njia ya kunyunyiza maji kidogo kichwani hauonyeshi kwa utoshelevu mfano huo wa kuzaliwa upya.

Je! Kufa pamoja na Kristo maana yake ni nini hasa?
"Tukijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulubishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena" - (Warumi 6:6)

Ubatizo unawakilisha kwa nje kile anachopaswa mtu kufanya ndani yake: yaani, kusalimisha kila kitu kwa Kristo. Tukizuia kitu chochote kwa Mungu, huenda tutaendelea kuwa " Watumwa wa dhambi" Tunapojisalimisha kabisa kwa Kristo, tamaa zetu za dhambi zinafanywa kuwa bila nguvu yoyote na badiliko kamili linaanza kutokea.

Je! Ni nani ahusikaye na mabadiliko yanayotokea?

Nimesulubiwa pamoja na Kristo wala mimi si hai tena, lakini KRISTO ANAISHI NDANI YANGU. Na maisha haya ninayoishi katika mwili huu, NAISHI KWA KUMWAMINI MWANA WA MUNGU, aliyenipenda na kujitoa nafsi yake kwa ajili yangu" - (Wagalatia 2:20).

Ninapojifananisha na kusulibiwa kwake Kristo kwa njia hiyo ya ubatizo nakaribisha uwezo wenye nguvu nyingi katika maisha yangu - yaani, " Kristo anaishi ndani yangu". Ili upate kuyaweka maisha yako mikononi mwa Kristo kabisa kwanza huna budi kumtazama Kristo akifa pale msalabani. Usiiangalie ile dhambi inayokutishia wewe, usiingalie kumbukumbu yako ya zamani na kuomboleza mtazame Yesu. Kukitazama kifo chake Kristo kilichojaa neema na ujasiri pale Kalvari, unaweza kuonyesha mshikamano wako ulio nao pamoja naye, kwa maneno haya: " Kwa nguvu ya msalaba nadai kwamba mimi ni mfu kwa zile tabia zangu za zamani, na Mungu. Naamua kusimama pamoja na Kristo. Kuanzia sasa na kuendelea mimi nita"ishi kwa kumwamwini aliyenipenda na kujitoa nafsi yake kwa ajili yangu"

Tunapoichota ile nguvu itokanayo na kifo na ufufuo wake Kristo, tunaziona sifa za tabia yake zikijitokeza zaidi na zaidi na kuchukua mahali pa tabia zetu zile za zamani:
"Mtu awaye yote akiwa NDANI YA KRISTO, amekuwa KIUMBE KIPYA: ya Kale yametoweka, MAPYA yamekuja!" - (2 Wakorintho 5:17).

Kwa njia hiyo ubatizo sisi tunaonyesha tamaa yetu tuliyonayo ya kushikana mikono na Yesu na kuishi hayo maisha mapya yaliyo bora tukiwa ndani ya Kristo" Yesu anafanya ndani yetu kile ambacho sisi tusingeweza kamwe kujifanyia wenyewe. Tunapanda kutoka ndani ya maji tukiwa " [vi]umbe [vi]pya" anatupa uwezo wa kuishi hayo "maisha mapya".

3. Hivi Kwa Nini Yesu Alibatizwa?

Wakati ule wa Pentekoste, Petro aliwaambia wale waliotaka kuwekwa huru mbali na dhambi kwamba wanapaswa kutubu na kubatizwa ili Kristo aweze kuwasamehe "dhambi zenu" (Matendo 2:38) Kwa kuwa Yesu hakutenda kamwe dhambi hata moja, basi kwa nini alijiachia mwenyewe kubatizwa?

"Wakati huo YESU AKAJA kutoka Galilaya MPAKA YORDAN ILI ABATIZWE na Yohana … KUITIMIZA HAKI YOTE" - Mathayo 3:13,15.

Yesu alikuwa hana dhambi. Hakuwa na haja ya kutubu dhambi yoyote. Alibatizwa kutokana na sababu nyingine: "Kutimiza haki yote" kwa kubatizwa kwake, Yesu alitoa kielelezo chenye nguvu kwa ajili yetu sisi wanadamu dhaifu na wenye dhambi. Kristo kamwe hawaombi wafuasi wake kwenda mahali kokote ambako yeye hajapata kufika. Kwa hiyo waumini wanapozamishwa ndani ya maji ya ubatizo, wanafuata nyayo za bwana wao.

Kwa vile Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, anaweza kutupa sisi haki yake.

Mungu alimfanya yeye asiyekuwa na dhambi kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili ndani yake sisi tupate kuwa haki ya Mungu" 2 Wakorintho 5:21.

Tukiwa tumebadilishwa kabisa kutoka katika hali yetu ya kuwa wenye dhambi na kuwa watakatifu machoni pake Mungu, tunakuwa ndani ya ile "haki" na kwa njia hiyo tunaishi maisha mapya ndani ya Kristo.

4. Kwa Nini Nizamishwe Ndani Ya Maji?

Kristo alizamishwa ndani ya maji wakati wa ubatizo wake. Hakunyunyiziwa maji kidogo kichwani. Yohana alimbatiza ndani ya mto wa Yordani "kwa sababu huko kulikuwa na MAJI TELE" (Yohana 3:23) Yesu alipobatizwa alikwenda na kuingia ndani ya maji, kisha "mara tu Yesu alipokwisha kubatizwa [alipokwisha kuzamishwa , Kigiriki] AKAPANDA KUTOKA NDANI YA MAJI" (Mathayo 3:16)

Tunapoielewa maana halisi ya ubatizo, hatuna shida sana kuutambua mfumo sahihi wa ubatizo. Neno lenyewe hasa la "ubatizo"linatokana na neno la Kigiriki baptizo " ambalo linamaanisha kuchovya au kuzamisha, kuweka chini ya).

Wakati wa ziara yake moja John Wesley kule Amerika katika mwaka wa 1737, baraza la wazee wa mahakama ya kanisa wapatao wanaume 34 walimhukumu yeye kwa shtaka la ajabu la "kukataa kumbatiza mtoto wa Bwana Parker, isipokuwa kwa njia ya kumzamisha ndani ya maji." Ni dhahiri kwamba baba huyo wa Kimethodisti aliwabatiza waongofu wake kwa kuwazamisha ndani ya maji.

Mwanamatengenezo ya kanisa John Calvin alieleza hivi: "Ni jambo la hakika ya kwamba kuzamisha majini ilikuwa ndiyo desturi ya Kanisa lile la kale" - Institute of the Christian Religion, Kitabu cha 4, Sura ya 15, Sehemu ya 19.

Historia ya kanisa lile la kwanza inadhahirisha kwamba ubatizo ulimaanisha kuzamishwa ndani ya maji.

Mkuu wa makasisi Stanley, wa Kanisa la Anglikana, aliandika maneno haya: "Kwa karne kumi na tatu za mwanzo, desturi ya ubatizo iliyoenea sana mahali pote ilikuwa ni ile tuisomayo katika Agano Jipya, na ambayo ndiyo
maana halisi ya neno "batiza" - kwamba wale waliobatizwa walitumbukizwa, yaani walifunikwa kabisa na maji, walizamishwa ndani ya maji" - Christian Institutions, Uk. 21

Mashimo ya kubatizia ndani ya maji yanaonekana katika makanisa mengi yaliyojengwa kati ya karne ya nne na karne ya kumi na nne kule Ulaya na Asia, makanisa kama vile kanisa Kuu la Pisa, Italiana la Mtakatifu Yohana, kanisa kubwa kuliko yote mjini Roma.

Kanisa Katoliki halikuukubali ubatizo wa kunyunyizia maji kichwani kuwa ni wa halali kama ule wa kuzamishwa majini mpaka lilipokaa Baraza la Ravena mapema katika karne ile ya kumi na tano. Katika masuala yale yanayohusu desturi za kanisa, hatutakiwi kufuata kile anachofundisha mwanadamu, bali kile ambacho Kristo na mitume wake wanafundisha.

Wakristo wengi waliowanyofu wa moyo wanayapenda sana yale mapokeo yahusuyo ubatizo wa watoto wachanga, na kule kuwatoa watoto wetu kwa Mungu kuanzia mwanzo kabisa wa maisha yao ni jambo linalopendeza hakika. Walakini, Biblia inaeleza wazi ya kwamba ni lazima mtu afundishwe ile njia ya wokovu kabla ya ubatizo wake (Mathayo 28:19,20) kwamba ni lazima mtu amwamini Yesu kabla ya kubatizwa (Matendo 8:35-38) na ya kwamba ni lazima mtu atubu dhambi zake na kusamehewa kabla ya kubatizwa (Matendo 2:38) Mtoto mchanga hana uwezo kabisa wa kuamini, kutubu au kuungama dhambi zake, mambo ambayo ni lazima yatangulie kabla ya ubatizo.

5. Kwa Nini Ni Muhimu Kubatizwa?

Kulingana na Yesu, ubatizo ni wa lazima kwa wale wanaotaka kuingia mbinguni.

"Hakuna mtu ye yote awezaye kuingia katika ufalme wa Mungu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho"- Yohana 3:5.

Yesu anatoa walakini mmoja tu. Yule mwizi pale msalabani ali"zaliwa kwa Roho" ingawa kwake ilikuwa haiwezekani kabisa hata kuondoka tu pale msalabani na kwenda kuzamishwa ndani ya maji kama ishara ya badiliko lake la moyo. Naye Yesu alimwahidi kwamba angekuwa pamoja naye [Kristo] katika ufalme wake (Luka 23:42,43) Kwa yule mwizi, kuzaliwa kwa maji na kwa Roho" kuliwakilishwa na damu ya Yesu iliyomwagika pale kumtakasa dhambi zake. Agostino (Augustine) alichunguza na kusema "Kuna tukio moja la toba ya mtu mmoja aliyekuwa akifa kitandani pake ambalo limewekwa katika kumbukumbu, yaani lile la mwizi yule aliyetubu, ili asiwepo mtu hata mmoja wa kukata tamaa, naye alikuwa ni yule mmoja tu ili asiwepo hata mmoja anayethubutu kufanya hivyo"

Yesu mwenyewe alitoa onyo hili zito:
Aaminiye na kubatizwa ataokoka, asiyeamini [na kwa sababu hiyo habatizwi]atahukumiwa " - Marko 16:16

Alipokuja badala yetu pale Kalwari Yesu alionyesha mbele ya wanadamu wote upendo wake alionao kwetu sisi. Tunahitaji kuitikia kwa kufanya ungamo letu bila haya mbele ya watu kuhusu kujitoa kwetu kwa Kristo kwa njia ya ubatizo. Je! Hivi wewe umeanza maisha hayo mapya ndani ya Kristo? Je! Umebatizwa ? Kama sivyo kwa nini wewe usijiandae kwa ubatizo katika siku za karibuni?

6. Ubatizo Ni Mwanzo Tu

Ubatizo unawakilisha kujitoa kwetu ili tupate kuishi mtindo wa maisha ya Kikristo. Lakini kule kujisalimisha kwetu wakati wa ubatizo hakujiendeshi kwenyewe kama mashine katika kipindi chote cha maisha yetu.

Mtoto anapozaliwa, kufanya sherehe ni sawa. Baada ya siku ya kuzaliwa kupita na msisimko kupungua, yule mtoto mchanga anahitaji kulishwa kila siku, kuogeshwa kila siku, na kuwa makini kila siku kuangalia afya yake.
Ni sawasawa na ubatizo. Paulo alisema hivi kuhusu uzoefu wake wa maisha "Ninakufa kila siku" (1 Wakorontho 15:31) Kwa kubadilika kila siku na kuachana na ubinafsi wetu, tunakuwa wepesi kuvutwa na zaidi kwa Kristo.

Taratibu ya ibada ya ubatizo, kama sherehe ya kufungisha ndoa, ilikusudiwa kuwa uthibitisho rasmi uonyeshao kwamba uhusiano wa ajabu ambao unakuwa umekwisha kuanza. Ili kuweza kukua daima tunahitaji kujitoa sisi wenyewe kila siku kwa Kristo kupokea kila siku maisha hayo mapya kwa njia ya maombi na kujifunza Biblia.

7. Sababu Ya Kushangilia

Ubatizo ni sababu iletayo kushangilia sana kwa sababu wale wanaomwamini Kristo wanayo ahadi ya uzima wa milele. Yeyote aaminye na kubatizwa ataokoka (Marko 16:16) Tunapokwisha kubatizwa tunaingia katika njia ile iendayo juu ambayo inatupeleka kwenye ile furaha ya milele.

Ubatizo pia unasherehekea furaha yetu tuliyo nayo sasa pamoja na Kristo. Anaahidi kuwapa zawadi ya thamani kubwa mno ya Roho Mtakatifu wale waliobatizwa (Matendo 2:38) Pamoja na huyo Roho huja lile "tunda la Roho" - yaani upendo ambao unayajaza maisha yao na "uvumilivu, utuwema, fadhili, uaminifu, upole na kujitawala nafsi" (Wagalatia 5:22,23)

Kuwa na Yesu anayeishi ndani yetu kwa njia ya Roho Mtakatifu hutupa sisi hisia kubwa sana ya kuwa na hakika. Kwa maana " Roho Mwenyewe hushuhudia … ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu" (Warumi 8:15,16)

Uhusiano huo imara pamoja na Mungu unatuletea manufaa mengi, lakini hautoi dhamana kwetu ya kutupatia maisha yasiyokuwa na matatizo yoyote.

Kwa kweli, adui yetu mara nyingi anajitahidi sana kuwatupia shida nyingi sana wale waliokwisha kujitoa sasa kwa Kristo. Walakini tunapokuwa
mikononi mwake Mungu tunaweza kujua kwamba atatumia kila jambo linalotupata sisi, liwe jema au baya, ili kutufundisha na kutusaidia kukua (angalia Warumi 8:28)

Mwanamke mmoja kijana alikata shauri kutoa maisha yake kwa Kristo na kubatizwa licha ya vitisho vya kumpa talaka toka kwa mume wake. Yeye hakutaka sehemu yoyote ya imani yake ile mpya lakini mwanamke yule akamng'ang'ania Yesu na kujitahidi kuwa mwenye upendo kuliko alivyokuwa kabla yake. Kwa kipindi fulani yule mume alifanya mambo kuwa magumu mle nyumbani. Lakini hatimaye alishawishiwa kwenda upande wa mkewe kutokana na hoja aliyoshindwa kuijibu: yaani, maisha ya mkewe yaliyobadilika kabisa. Mtu huyo akasalimisha maisha yake kwa Kristo, naye akabatizwa pia.

Kule kung'ang'ania kwetu kusimama karibu na Kristo "kwa heri na kwa shari" [katika hali iwayo yote ile] kutatufanya kuwa vyombo vyenye nguvu nyingi mikononi mwake. Tunaweza kumkabidhi maisha yetu bila masharti yoyote kwa sababu yeye kimsingi tayari amekwisha kujitoa kwetu alipolipa fidia kwa ajili ya dhambi zetu pale msalabani. Ni heshima kubwa iliyoje tuliyopewa sisi kuweza kumpa upendo na utii wetu mbele ya watu! Endapo wewe bado hujafanya hivyo, kwa nini usisalimishe maisha yako kwa Kristo sasa hivi. Mwombe yeye akupe maisha mapya ndani yako kwa njia ya Roho wake Mtakatifu halafu batizwa na kuingia ndani ya Kristo.

 

© 2004 The Voice of Prophecy Radio Broadcast
Los Angeles, California, U.S.A.