SIRI YA FURAHA

Mwaka 1943, majeshi ya Uvamizi ya Kijapani yaliwaamuru wale "Wananchi Maadui" wa Kimarekani na Ulaya kwenda katika kambi la waliotekwa vitani katika lile Jimbo la china la Shantung.

Walilazimika kustahimili miezi mingi ya kuchosha sana, ya kukata tamaa, ya kusongamana pamoja na ya hofu. Watu wenye tabia tofauti waligongana, hasira zililipuka. Magomvi madogo madogo yaliongezeka sana.

Lakini mtu mmoja alielezwa na mfungwa mmoja wa kivita kwamba "bila shaka lolote alikuwa ni mtu aliyehitajika sana na kuheshimiwa sana, tena aliyependwa sana katika kambi lile. "-Eric Liddell, Mmishonari kutoka katika nchi ya Waskoti (Scotland).

Malaya mmoja wa Kirusi katika kambi lile baadaye aliweza kukumbuka ya kwamba yule Liddell ni mwanaume peke yake aliyeweza kumtendea yule mwanamke jambo lolote bila kutaka kulipwa kimwili. Mwanamke yule alipokuja mle kambini kwa mara yake ya kwanza, akiwa peke yake, na mwenye kudharauliwa, ndiye aliyemtengenezea yeye baadhi ya rafu za kuwekea vitu vyake.

Mfungwa wa vita mwingine alikumbuka kwamba, "yeye alikuwa na mbinu ya upole, na ya kuchekesha iliyozilainisha hasira zao zilizovurugika vibaya".

Katika mkutano mmoja uliojaa hasira wa wafungwa wale wa kivita, kila mmoja alikuwa akitoa madai yake kwamba mtu fulani mwingine ndiye angefanya kitu fulani kwa wale vijana watukutu wenye umri wa kuanzia miaka kumi na mitatu hadi kumi na tisa (matineja) ambao walikuwa wanajitia katika matatizo. Liddell akatoa suluhisho lake. Aliandaa michezo ya kujiburudisha, ufundi wa kutengeneza vitu kwa mikono, na madarasa kwa ajili ya watoto wale, na kuanza kutumia wakati wake wa jioni pamoja nao.

Liddell alijipatia sifa na utukufu katika Michezo ya Olimpiki ya mwaka wa 192, alijinyakulia nishani ya dhahabu katika mbio za mita 400. Lakini katika uwanja ule mdogo sana wa kambi lile alijionyesha pia ya kuwa ni mshindi katika zile mbio za Kikristo, akajipatia sifa kutoka kwa wafungwa wa vita wale walioipenda sana dunia hii.

Je! Ni kitu gani kilichomfanya kuwa mtu wa aina yake? Ungeweza kuwa umeigundua siri yake saa 12 kila asubuhi. Ule ndio wakati alipotoka kimya kimya kwa kunyatia akiwapita wenzake waliolala usingizi, na kutulia kimya mezani, na kuiwasha taa ndogo ili itoe mwanga wa kumwezesha kuliona daftari lake ndogo na Biblia yake. Eric Liddell alitafuta neema na nguvu kila siku kutoka katika utajiri wa Neno la Mungu.

1. Kitabu Cha Mwongozo Wa Kuishi Mtindo Wa Maisha Ya Kikristo

Biblia iliandikwa kama kitabu cha Mwongozo kwa Mkristo. Kimejaa visa vingi vya watu halisi walio kama sisi waliokabiliwa na changamoto zile zile tunazokutana nazo kila siku. Kuwafahamu wahusika hao wa Biblia - furaha na huzuni zao, matatizo yao na nafasi zao nzuri walizopata hutusaidia sisi kukomaa kama Wakristo.

Mtunga Zaburi, Daudi aonyesha mfano wa kulitegemea Neno la Mungu kila siku kwa kulilinganisha na mwanga wa tochi (kurunzi);
"Neno lako ni taa ya miguu yangu na mwanga wa njia yangu." Zaburi 119:105. (Isipokuwa pale ilipoelezwa vinginevyo, mafungu yote ya Maandiko katika GUNDUA Miongozo yanatoka katika Toleo Jipya la Kimataifa la Biblia - New International Version (NIV).

Nuru tunayoipata kila siku kutoka katika Biblia inafunua wazi sifa zile tunazozihitaji katika maisha yetu na kanuni za kukua kiroho. Zaidi ya hayo yote, Biblia inatuonyesha Yesu, Nuru ya Ulimwengu. Maisha yetu yana maana tu anapoyaangazia Yesu kwa Nuru yake.

2. Urafiki Unaotubadilisha Kabisa

Kristo anataka Biblia kwako iwe kama barua uliyoandikiwa mwenyewe itokayo kwa rafiki yako wa karibu sana.

"Ninyi nimewaita rafiki, kwa sababu kila kitu nilichokisikia kwa Baba nimewajulisheni." - Yohana 15:15.

Yesu anatutakia mema matupu. Neno lake linatuingiza sisi katika familia ile ya ndani ya Mungu; Yaani, ya wale anaowaambia siri zake na kuwafundisha yeye mwenyewe.

"Nimewaambieni ninyi mambo hayo, ili ndani yangu ninyi mweze kuwa na amani." - Yohana 16:33.

Ili kuweza kuionja amani hiyo, na uhusiano huo thabiti pamoja na Kristo, ni lazima tuzisome barua zake anazotutumia. Hivyo ndivyo Biblia ilivyo: ni barua zitokazo mbinguni. Usiziache barua hizo bila kuzifungua. Ujumbe uwezao kuyabadilisha kabisa maisha yako ambao unauhitaji umo ndani ya Neno hilo.

Hapa upo ushuhuda mmoja kamili uhusuo matokeo ya kuisoma Biblia. "Mimi nilihitaji msaada, nao niliupata ndani ya Yesu. Kila haja yangu ilitimizwa, njaa ya nafsi yangu ilishibishwa; kwangu Biblia ni ufunuo wake Kristo. Namwamini Yesu kwa sababu yeye kwangu ni Mwokozi wa Kimbingu. Naiamini Biblia kwa sababu nimeiona kuwa ni sauti ya Mungu rohoni mwangu. " - The Ministry of Healing, uk. 461.

3. Miongozo Ya Kuishi Kwa Kufuata Biblia Na Zile Amri Kumi

Kuziangalia kwa kifupi tu hizo Amri Kumi kutatusaidia kuelewa kwa nini hizo pamoja na Biblia hujenga msingi muhimu sana wa maisha yaliyo manyofu.

Amri hizo kwa kawaida huangukia katika sehemu kuu mbili. Zile nne za kwanza hufafanua uhusiano wetu na Mungu, na zile sita za mwisho hufafanua uhusiano wetu na watu wengine. Zinapatikana katika Kutoka 20:3-17.

Amri mbili za kwanza zinaelezea uhusiano wetu na Mungu pamoja na ibada yake.

I. "Usiwe na Miungu mingine ila Mimi".
II. "Usijifanyie sanamu ya kuchonga. Usizisujudie wala kuzitumikia…"

Amri ile ya 3 na ya 4 hueleza kwa juu juu tu uhusiano wetu na jina la Mungu na siku yake takatifu.

III. "Usilitaje bure jina la BWANA, Mungu wako…"

IV. "Ikumbuke siku ya Sabato uitakase. Siku sita fanya kazi, utende mambo yako yote, lakini siku ya saba ni Sabato ya BWANA, Mungu wako…"

Amri ya 5 na ya 7 inaimarisha vifungo vya familia.

V. "Waheshimu baba yako na mama yako…."

VI. "Usizini."

Amri ya 6, 8, 9 na 10 hutulinda sisi katika uhusiano wetu kijamii.

VII. Usiue."

VIII. "Usiibe."

IX. "Usimshuhudie jirani yako uongo."
X. "Usiitamani nyumba ya jirani yako. Usimtamani mke wa jirani yako….. wala chochote alicho nacho jirani yako."

Amri hizo kumi zinaweka mipaka ya uhusiano wetu kwa Mungu na kwa watu wengine. Hizo ni nguzo za kutuongoza katika mtindo wa maisha yetu ya Kikristo.

4. Aliyosema Yesu Juu Ya Hizo Amri Kumi

Siku moja Yesu alipokuwa akifundisha, kijana mmoja mwanaume mwenye ari kubwa aliharakisha kwenda kwake na kumwuliza, "Mwalimu, nitende jambo gani jema ili nipate uzima wa mielel?" (Mathayo 19:16). Yesu aliweza kuona yule kijana alikuwa akipambana na tatizo la fedha, ndipo akamshauri kuachana na mali yake na ku"zishik(a) amri" (fungu la 17).

Yule kijana mwanaume alijaribu kuukwepa utambuzi wa tatizo lake alioufanya Kristo kwa kuuliza ni amri zipi alizokuwa akiziongelea. Yesu akaorodhesha amri kadhaa katika zile Amri kumi (fungu la 18, 19).

Mwishowe, yule "mtawala kijana tajiri" aligeuka na kwenda zake kwa huzuni (mafungu ya 20-22). Kiakili yeye alizikubali zile Amri kumi, ila hakuweza kuitii roho ya ile Sheria kwa kuachana na njia yake ya maisha ya uchoyo.

Amri kumi zinatuonyesha sisi mipaka ambayo ndani yake unaweza kukua uhusiano wenye afya pamoja na Mungu na kila mmoja wetu. Yesu alisonda kidole chake kwenye utii kuwa huo ndiyo njia ya kuipata furaha ya kweli.

"MKIZISHIKA AMRI ZANGU, mtakaa katika pendo langu, kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Mimi NIMEWAAMBIA NINYI ILI furaha yangu iwe ndani yenu, na FURAHA YENU IWE KAMILI." Yohana 15:10,11.

5. Mwongozo Kwa Maisha Yenye Furaha

Kitabu cha Mhubiri ni taarifa ya utafiti wa Sulemani juu ya furaha. Anaandika kumbukumbu ya safari zake za kutafuta furaha katika utajiri wa ulimwengu huu, nyumba za kifahari, mashamba ya mizabibu izaayo sana, bustani nzuri sana, na mashamba ya miti ya matunda matamu sana yenye harufu nzuri. Aliongeza idadi ya watumishi wake. Alijikuta amezungukwa na kila kitu ambacho mtu angeweza kukitamani. Lakini furaha ikateleza na kwenda mbali naye, ndipo akaandika, akasema. "Nilipozichunguza kazi zote zilizokuwa zimefanywa na mikono yangu, na kusumbuka kwangu kote katika kuzitenda, kila kitu kilikuwa hakina maana kabisa, ilikuwa ni sawa na kujilisha upepo" - (Mhubiri 2:11).

Ndipo Sulemani alipogeuka ili kuzitafuta anasa za ulimwengu huu kwa tumaini la kuipata furaha. Akatawaliwa na mvinyo, wanawake, na nyimbo. Hitimisho lake ni hili:
"Bure kabisa, bure kabisa, nakuambia mimi, Mhubiri! Kila kitu ni bure kabisa" (Mhubiri 12:8.

Zamani Sulemani alikuwa amepata kuonja na kuona ya kuwa Bwana yu mwema. Alipoyalinganisha maisha yake yale ya kwanza ya utii wake kwa Mungu na maisha yake ya kutafuta furaha katika mambo ya dhambi bila kujali kitu, wosia wake ukawa ni huu:
"Hili ndilo hitimisho la jambo hilo: Mche Mungu, na kuzishika amri zake, kwa maana huo ndio wajibu wote umpasao mtu." - Mhubiri 12:13.

Sulemani aliona angeweza kutafuta njia ya mkato ya kupata furaha kwa kuishi maisha mapotovu. Karibu na mwisho wa maisha yake, alikuwa mwanaume tosha kuweza kukiri kosa lake. Ili kuwaokoa wengine wasitende kosa lile lile, aliandika maneno haya, "Yule aitunzaye Sheria, ana furaha." Mithali 29:18, KJV.

6. Amri Kumi Ni Mwongozo Muhimu Sana Wa Agano Jipya

Katika Agano jipya, Yakobo alitoa ushuhuda wake huu:
"Maana yeyote anayeishika sheria yote, lakini anajikwaa katika neno moja tu ana hatia ya kuivunja yote. Kwa maana yeye aliyesema; "Usizini, pia alisema, "Usiue", Usipozini, lakini ukiua, umekuwa mvunja sheria. Semeni ninyi, na kutenda kama watu wale watakaohukumiwa kwa sheria inayowapa uhuru. "Yakobo 2:10-12.

Charles Spurgeon, Mhubiri Mkuu wa Kibaptisti wa karne iliyopita alitangaza akisema." Sheria ya Mungu ni Sheria ya Mbinguni - takatifu, ya Mungu, na kamilifu---- Hakuna amri yake hata moja iliyozidi kiasi; hakuna amri yake hata moja iliyopungua mno, lakini yenyewe haina kifani kiasi kwamba ukamilifu wake ni uthibitisho wa Uungu wake." John Wesley, mmojawapo wa Waasisi wa Kanisa la Methodisti, aliandika maneno haya juu ya tabia ya kudumu ya sheria hiyo. "Sheria hiyo ya Maadili iliyo katika hizo amri kumi…. Yeye (Kristo) hakuiondoa…. Kila kipengele cha Sheria hiyo ni lazima kiendelee kuwa na nguvu juu ya wanadamu wote na katika vizazi vyote…. Sermons, gombo la 1, kurasa 221,222.

Billy Graham, Mwinjilisti wa Kiinjili wa Ulimwengu mzima aliyeheshimiwa sana, anaziheshimu sana Amri kumi kiasi kwamba ameandika kitabu kizima juu ya umuhimu wa amri hizo kwa Mkristo.

7. Uwezo Wa Kutii

Biblia pamoja na zile Amri Kumi ni mwongozo usiobadilika, wa muhimu sana, na mkamilifu uletao maisha yenye furaha. Lakini, basi, mioyo ya watu bado inayo mapambano ndani yake. Mwanamke mmoja alijieleza kama ifuatavyo: "Mimi naamini kwamba hizo Amri kumi zinawafunga watu wote, nina hakika kwamba kuzishika huleta furaha. Nimejitahidi kwa nguvu zangu zote kuzishika, lakini siwezi kuzishika. Ninaanza kuamini kwamba hakuna mtu mwingine awaye yote anayeweza kuzishika."

Mwelekeo wa asili wa mtu ni kujaribu kuishi maisha hayo ya utii kwa hizo amri za Mungu. Lakini kujitahidi kama huko, tena na tena, kunakotoka katika moyo wenye dhambi wa mtuhuleta jibu hili la kukatisha tamaa, "Mimi siwezi kutii!" kwa nini? Kwa sababu.

"Nia yenye dhambi ina uadui na Mungu. Haitii sheria ya Mungu, wala haiwezi kuitii." Warumi 8:7.

Je! Kusudi la sheria hiyo ya Amri kumi ni nini?
"Kwa njia ya sheria (Amri kumi) sisi tunaitambua dhambi." Warumi 3:20.

Kazi ya sheria (Amri Kumi) ni kutufanya tutambue kabisa kwamba sisi" tu wenye dhambi tuliopotea na kuwa bila tumaini, ambao tunamhitaji Mwokozi.

"Sheria (Amri kumi na Sheria ya Kafara) ilipewa madaraka juu yetu kutuongoza kwa Kristo ili tupate kuhesabiwa haki kwa imani." - Wagalatia 3:24.

Yesu ndiye jibu! Mara tu sisi tunapokuwa miguuuni pake Yesu, tukiwa hatuna uwezo wowote kabisa, tunaweza kupokea msamaha kwa ajili ya dhambi zetu, pamoja na uwezo toka kwake utakaotuwezesha kuzitii amri zake kwa njia ya imani.

8. Utii Kwa Amri Kumi Utokanao Na Upendo

Yesu anatuambia kwamba utii ni matokeo ya upendo.

"Mkinipenda, mtazishika amri zangu" - Yohana 14:15.

Tukimpenda Mungu, tutazitii amri zile nne za kwanza zinazofafanua uhusiano wetu na Mungu; na kama tukiwapenda watu, basi, tutazitii zile sita za mwisho ambazo hufafanua uhusiano wetu na wengine.

Mtu awaye yote anayezikanyaga Amri Kumi chini ya miguu yake anatenda dhambi.

"Kila mmoja atendaye dhambi anaivunja sheria (Amri Kumi); ukweli ni kwamba, dhambi ni uvunjaji wa sheria (Amri kumi)," 1Yohana 3:4.

Lakini Mungu na ashukuriwe, tunaye Mwokozi aliyekuja katika dunia hii na kufa, alifufuliwa, na sasa yu hai kwa ajili ya kusudi moja tu:
"Lakini ninyi mnajua ya kwamba alikuja ILI AZIONDOE DHAMBI ZETU."- Fungu la 5.

Ndani yetu hatuna uwezo wowote kutuwezesha kuishika hiyo sheria ya Mungu (amri kumi). Upendo wa Mungu "uliomwagwa…. Ndani ya mioyo yetu" ndilo tumaini letu la pekee.

9. Neema Ya Mungu Na Utii Wetu Kwa Sheria Yake

Wokovu ni zawadi. Hatuwezi kuufanyia kazi ili tuweze kustahili kuupata. Tunaweza tu kuupokea kwa imani. Tunakupokea huko kuhesabiwa haki (kuwa katika msimamo sahihi na Mungu) kama zawadi; kwa njia ya imani peke yake kwa sababu ya neema yake Mungu.

"Kwa maana MMEOKOLEWA KWA NEEMA, kwa njia ya IMANI-na hiyo haitokani na nafsi zenu wenyewe, ni ZAWADI TOKA KWA MUNGU - Si kwa matendo, mtu yeyote asije akajisifu" Waefeso 2:8.

Hatuwezi kuzishika amri hizo kwa matendo yetu wenyewe - yaani, kwa kujitahidi kwetu. Hatuwezi kuzishika amri hizo ili tupate kuokolewa. Lakini tunapomwendea Yesu kwa imani na unyenyekevu na kuokolewa naye, hapo ndipo upendo wake unaijaza mioyo yetu. Kama matokeo ya neema hiyo ya Mungu na kukubaliwa naye, sisi tunaingiwa na shauku ya kumfuata yeye na kumtii kwa njia ya uwezo wa upendo wake ulio ndani ya mioyo yetu (Warumi 5:5).

Paulo anatilia mkazo wake juu ya kutokufaa kabisa kwa juhudi za kibinadamu, naye anadokeza kwamba sisi hatuko chini ya sheria kama njia ya kujipatia wokovu wetu, bali tuko "Chini ya neema."

"Je! Tutende dhambi (tuzivunje Amri kumi) kwa sababu hatuko chini ya sheria (amri kumi) bali chini ya neema? Hasha!" - (Warumi 6:15).

Kwa nini? Kwa sababu moyo ule unaosukumwa na upendo unazaa maisha ya utii utokanao na upendo huo! (Warumi 13:10). Kumpenda Kristo ni kumtii yeye.

"Yeye aliye na amri (kumi) zangu na kuzitii, ndiye anipendaye mimi." Yohana 14:21.

Eric Liddel alidhihirisha kwamba, hata katika mazingira mabaya sana, muumini aliyepewa uweza wa Mungu unaweza kuishi maisha ya kuridhika, maisha ya utii. Liddell alionyesha wazi tabia yake iliyowavutia watu katika kipindi kile cha dhiki na hofu. Uhusiano wake wa upendo kwa Kristo ulimtia nguvu kwa njia ya Roho Mtakatifu, na kumwezesha kuyatimiza "matakwa ya haki yanayodaiwa na sheria" (Warumi 8:1-4). Uhusiano wa upendo na yule Mwokozi aliyesubiliwa na kufufuka unaweza kuzaa aina hiyo ya maisha.

Je! Hivi wewe umeigundua mwenyewe siri hii? Upendo wa Kristo kwa ajili yako ulimfanya atoe maisha yake kwa ajili ya dhambi yako. Yeye anajitolea kuutia nguvu uhusiano wako wote kwa kukupa upendo wake na kuku "fan(ya) (wewe) kuwa (m) kamilifu katika kila tendo jema ili upate kutenda mapenzi yake" (Waebrania 13:12). Jibu lako ni lipi?


© 2004 The Voice of Prophecy Radio Broadcast
Los Angeles, California, U.S.A.