UWEZO WA AJABU KATIKA MAISHA YANGU

Katika mwaka ule wa 1929 (Frank Morris) alipanda meli iliyokuwa ikienda Uswisi. Alikuwa ametazamia kufanya safari ile kwa muda fulani. Lakini ikageuka na kuwa safari ya kumdhalilisha. Mtumishi aliyewekwa kumtunza alimfungia Frank katika chumba chake kila siku. Baada ya kupata kifungua kinywa, kwa haraka-haraka Frank aliweza kufanya mazoezi ya viungo kidogo, lakini yeye alijisikia kana kwamba alikuwa mpumbavu kuweza kuongozwa vile huku na huku juu ya sitaha ya meli ile, kama vile yeye alikuwa mnyama anayeongozwa kwa kamba. Wakati wo wote alipokutana na abiria aliyeonyesha urafiki kwake na kumwalika kwenda kutembea naye, yule mtumishi alikataa, akawaambia kwamba alipaswa kumwangalia kila wakati.

Frank alikuwa mtu mzima, mwenye hisia za kawaida za udadisi na tamaa anazopaswa kuwa nazo mtu mzima. Lakini yeye alikuwa kipofu pia. Yule mtumishi alidhani kwamba asingeweza kujitunza mwenyewe. Frank alitendewa kana kwamba alikuwa kifurushi vile, kilichopaswa kuburutwa huku na huku.

Lakini katika nchi ile ya Uswisi maisha ya Frank yalibadilika kwa namna ya kuvutia sana. Alipokuwa kule alijifunza habari za mbwa waliokuwa wamepewa mafunzo ya kuwaongoza vipofu. Aliporudi kule Marekani pamoja na kiongozi [mbwa] wake wa safari wa Kijerumani aliyeitwa Buddy, Frank alianzisha Jicho Lionalo, sasa ni shirika lililoenea ulimwenguni kote.

Sasa Frank, akiwa na Buddy kando yake, aliweza kwenda ko kote, wakati wo wote, na mtu ye yote. Hatimaye alijisikia huru. Katika maonyesho yake ya kwanza kwa waandishi wa habari penye njia panda yenye magari mengi katika lile Jiji la New York, yule Buddy alimwongoza bwana wake kwa ustadi kutoka katika njia moja na kuingia katika njia nyingine wakati yale magari yalipokuwa yakiunguruma na kupita. Kwa kuwa yeye alimtumainia yule Buddy, Frank alivuka kwa urahisi mpaka upande ule wa pili. Waandishi wa habari walioonekana pale walikuwa na wakati mgumu zaidi kuvuka pale; mmoja wao alichukua kabisa teksi ili kwenda upande ule wa pili.

Katika kurasa chache zifuatazo tunakwenda kujifunza juu ya Roho Mtakatifu, kiongozi anayetaka sisi tuyakabidhi maisha yetu mikononi mwake. Sisi sote tumelemaa kutokana na asili yetu moja ya kibinadamu, tunao upofu ule ule katika mambo yale yaliyo ya maana sana kwetu. Maisha yetu hupita kasi kwa namna ambayo tunajikuta wenyewe tunayavumilia tu badala ya kwenda mahali fulani. Hata hivyo, sisi tunasita-sita kuyakabidhi maisha yetu kikamilifu kwa Kiongozi huyo. Lakini ugunduzi unaomngojea kila mmoja wetu ni huu: sisi tutapata uhuru wa kweli na uwezo kwa kumtegemea Roho Mtakatifu kutuongoza katika maisha yetu yote.

1. Mwakilishi Wa Kristo Ulimwenguni

Kristo alipokuwa tayari kupaa kwenda mbinguni, aliwaahidi wanafunzi wake kwamba atawapa zawadi ya thamani kuu isiyokadirika:
"Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke kwa maana nisipoondoka huyo MSAIDIZI hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu. Lakini atakapokuja, HUYO ROHO WA KWELI, ATAWAONGOZA awatie kwenye kweli yote…. YEYE ATANITUKUZA MIMI kwa kuwa atatwaa katika yaliyo yangu na kuwapasha habari". - (Yohana 16:7,13,14).

Katika mpango wa Mungu, Yesu alihitaji kurudi mbinguni kuwa Mwakilishi wetu mbele ya kile kiti cha enzi cha Mungu ili "aonekane sasa usoni pa Mungu" (Waebrania 9:24). Wakati Bwana wetu aliyesulubiwa anapotuwakilisha sisi kule mbinguni, tunaye pia Roho Mtakatifu kama MSHAURI wetu na KIONGOZI wetu hapa hapa duniani. Yeye moja kwa moja ndiye Mwakilishi wa Yesu hapa.

Yesu alipokuwa hapa alifanya kazi zake akiwa amefungwa na mwili huu wa kibinadamu, tena yeye asingeweza kuwa kila mahali. Lakini huyo Roho Mtakatifu hana mipaka kama hiyo inayomzuia; ana weza kuhudumu kama Mshauri na Kiongozi kwa watu wasiohesabika walio mahali pengi kwa wakati mmoja. Kristo anakidhi mahitaji yetu kwa njia ya huyo Roho Mtakatifu.

2. Roho Mtakatifu Ni Nani?

Wengi wetu tunaweza kuwa na uhusiano wetu na Mungu Baba kama sisi tunatafakari habari za mzazi wetu tuliyepata kumjua ambaye alitutunza na kutulea vizuri sana. Tena mawazoni mwetu tunaweza kuona picha ya Yesu Mwanawe, kwa sababu yeye aliishi kati yetu kama mwanadamu. Lakini Roho Mtakatifu ni vigumu zaidi kuiona picha yake na kujenga uhusiano naye. Hatuna mifano rahisi ya kibinadamu ya kumlinganisha nayo. Walakini, Biblia inatoa habari za pekee zinazomhusu huyo Roho Mtakatifu:

Ni nafsi Mashuhuri. Yesu alimtaja huyo Roho Mtakatifu kama nafsi, mmojawapo katika ule Uungu, akiwa pamoja na Mungu Baba na Mungu Mwana:
"Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la BABA, na MWANA, na ROHO MTAKATIFU" - (Mathayo 28:19).

Roho huyo anazo tabia za kibinafsi: yeye anayo NIA (Warumi 8:27); HEKIMA (1Wakorintho 2:10); anazo HISIA ZA UPENDO kwetu sisi (Warumi 15:30); anajisikia HUZUNI tunapotenda dhambi (Waefeso 4:30); anao uwezo wa KUTUFUNDISHA sisi (Nehemia 9:20); na uwezo wa KUTUONGOZA sisi.

Alihusika katika uumbaji. Huyo Roho Mtakatifu alishirikiana pamoja na Baba na Mwana katika kuiumba dunia yetu hii.

"Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na dunia… Roho wa Mungu alitembea juu ya uso wa maji" - (Mwanzo 1:1,2,KJV).

3. Kazi Za Roho Mtakatifu

(1) Huugeuza Moyo wa Mwanadamu. Katika kukutana kwake na Nikodemo, Yesu aliikazia sana kazi ya Roho Mtakatifu ya kuubadilisha moyo wa mwanadamu.

"Yesu akajibu, Amini, Amini nakuambia, mtu asipozaliwa kwa maji na kwa roho hawezi kuingia ufalme wa Mungu" - (Yohana 3:5).

Kuzaliwa kwa Roho" maana yake ni kwamba huyo Roho anatupatia sisi mwanzo mpya. Ni zaidi ya kuibadilisha kidogo hapa na pale tabia yetu. Huyo Roho anatubadilisha sisi kuanzia ndani kwenda nje, akitimiza ahadi hii, "Nami nitawapa ninyi moyo mpya" (Ezekieli 36:26).

(2) Hutuwezesha sisi kuyatambua matendo yetu mabaya na kutupatia shauku ya kuwa na utakatifu:
"Naye [Roho Mtakatifu] akiisha kuja, huyo ATAUHAKIKISHIA ULIMWENGU kwa habari ya DHAMBI na HAKI na HUKUMU" - (Yohana 16:8).

Unaposikia kisa cha kusisimua juu ya mtu fulani anayeachana na maisha ya uasherati na kumgeukia Mungu na kuwa mwaminifu kwa mke au mume wake na kuwa mzazi anayejua kulea watoto, kumbuka kwamba kila hatua aliyochukua kuelekea kwenye uzima ilikuja kutokana na msukumo wa Roho Mtakatifu.

(3) Hutuongoza sisi katika maisha ya Kikristo. Yesu anazungumza nasi moja kwa moja kupitia kwa ile "sauti ndogo" ya huyo Roho.

"Na masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii ifuateni; mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto" - (Isaya 30:21).

Kwa njia ya matangazo ya Satelaiti, televisheni zetu zinatuletea daima katika sebule yetu picha na sura mbali mbali kutoka katika bara lililo mbali nasi. Roho Mtakatifu kwa kiasi kidogo anafanya kazi yake kama Satelaiti ya Mungu, akituletea kuwako kwake Kristo kutoka mbinguni kuja hapa duniani, na kumfanya awe karibu sana nasi wakati ule tunapomhitaji sana (Yohana 14:15-20).

(4) Hutusaidia sisi katika maisha yetu ya sala.
"Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Na yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo Mungu " - (Warumi 8:26,27).

Tunapojitahidi sana kutafuta maneno yanayofaa, Roho anatuombea sisi. Tunapokuwa tumekata tamaa kiasi cha kuweza kupiga kite [kuguna] tu kwa Mungu, Roho anakikuza kilio chetu hicho kinyonge tunachotoa ili kuomba msaada kwake na kukifanya kiwe sala yenye nguvu mbele kabisa ya kile kiti cha enzi cha Mungu pale mahali anapoendelea kuhudumu Yesu sasa.

(5) Kukuza Sifa na Tabia ya Kikristo. Roho anawafanya watu wale walio kama jangwa kiroho kuwa kama mti ulio na rutuba, uzaao aina zote za matunda: "LAKINI TUNDA LA ROHO ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole na kujitawala" - (Wagalatia 5:22,23).

Kuwa na tunda la Roho huonyesha kwamba sisi tunapandikizwa katika ule Mzabibu wa kweli, yaani, Yesu (Yohana 15:5). Yesu anaweza kuishi kabisa maisha yake tele kupitia kwetu kwa njia ya uweza wa huyo Roho.

(6) Hututayarisha sisi kuwa mashahidi wake. Yesu anatoa ahadi hii:
"LAKINI MTAPOKEA NGUVU akiisha kuwajilia juu yenu Roho Matakatifu; nanyi mtakuwa MASHAHIDI WANGU…. Hata mwisho wa nchi" - (Matendo 1:8).

Wale wote wanaotaka wanaweza kufanywa mashahidi wake kwa njia ya huyo Roho. Huenda sisi tusiweze kupata majibu yote, lakini huyo Roho anaweza kutupa sisi kisa fulani cha kusimulia kinachoigusa mioyo na akili za watu. Mitume wale walipata shida ya kuwasiliana na watu wale kabla ya Pentekoste, lakini baada ya yule Roho kuwajia, walimtangaza Kristo kwa uwezo uliowafanya wa "upindue ulimwengu" (Matendo 17:6, KJV).

4. Karama Za Roho

Maandiko yanaweka tofauti iliyo dhahiri kati ya kipawa cha Mungu cha Roho Mtakatifu ambacho anakitoa kwa KILA MUUMINI ili kumwezesha kuwa na maisha ya Kikristo yenye ushindi, na zile karama mbali mbali za Roho zinazotolewa kwa waumini ili wapate kutoa huduma yao kwa watu iletayo matokeo mazuri kwa kutumia njia mbalimbali.

"Hivyo husema [Kristo] alipopaa juu, aliteka mateka akawapa wanadamu vipawa. Naye alitoa WENGINE kuwa MITUME, na wengine kuwa MANABII, na wengine kuwa WAINJILISTI, na wengine kuwa WACHUNGAJI na WAALIMU,kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke hata mwili wa Kristo ujengwe" - (Waefeso 4:8, 11-12).

Si kila Mkristo anayepokea karama hizo zote, wengine wanaweza kupokea karama nyingi kuliko wengine; Roho ndiye "humpa kila mtu, kipaji tofauti kama apendavyo mwenyewe" (1 Wakorintho 12:11). Roho ndiye anayemtayarisha kila muumini ili apate kufanya sehemu yake maalumu katika mpango wa Mungu. Mungu anajua ni lini na ni wapi aweze kutoa karama zitakazowaletea mibaraka mingi sana watu wake na kanisa lake.

Orodha ya karama za Roho inayopatikana katika 1 Wakorintho 12:8-10 naijumuisha hekima, maarifa, imani, karama za kuponya, unabii, kunena kwa lugha mbali mbali, na kutafsiri lugha (fungu la 8-10).

Paulo anatusisitizia kutaka sana karama zilizo kuu," halafu anaongeza kusema, "Hata hivyo nawaonesha njia iliyo bora." (1 Wakorintho 12:31). Sura ile ya upendo (1 Wakorintho 13) ambayo inakuja baada ya fungu hilo inatilia mkazo kwamba "lililo kuu kupita yote" ni upendo. Na huo upendo ni tunda la Roho (Wagalatia 5:22).

Tungejishughulisha sana kulitafuta hilo tunda la Roho, halafu kumwacha Roho atugawie karama zake kama "anavyopenda mwenyewe" (1Wakorintho 12:11).

5. Utimilifu Wa Roho Wakati Wa Pentekoste

Siku ile ya Pentekoste, Roho alimwagwa kwa kipimo kisicho na mpaka, ili kutimiza ahadi ya Yesu:
"Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu… hata mwisho wa nchi." - Matendo 1:8.

Wakati wa Pentekoste Roho aliwawezesha wale mitume kuhubiri injili wazi wazi katika lugha za watu "wa kila taifa chini ya mbingu" (Matendo 2:3-6).

Baadhi ya wanafunzi wa Biblia hulinganisha kuja kwake Roho na mvua zinazonyesha mapema katika majira ya kupukutisha (autumn) na mvua zile za mwisho katika majira ya kuchipua (spring) katika nchi ya Palestina (Yoeli 2:23). Roho yule aliyemwagwa siku ile ya Pentekoste alifanana na"mvua ya kwanza" ya majira ya kupukutisha ambayo ilizifanya mbegu kuota na kulipa lishe muhimu kanisa la Kikristo katika uchanga wake.

6. Mvua Ya Masika Ya Roho

Unabii wa Biblia unatuambia habari za siku inayokuja ambayo katika hiyo Roho wa Mungu atamwagwa kama manyunyu ya mvua juu ya kanisa lake, akiwatia nguvu washiriki wa kanisa na kuwafanya mashahidi (Yoeli 2:28,29). Karne nyingi mpaka sasa zimekwisha kupita na habari ya wokovu imeenea katika sehemu kubwa ya ulimwengu huu. Sasa wakati umefika kwa "mvua ya masika" kunyesha ili kuzikomaza mbegu zilizoota, na kufanya nafaka iwe tayari kuvunwa.

Historia inapokwenda kufikia mwisho wake muda mfupi tu kabla ya Kristo kuja mara ya pili, Mungu atamfanya kila muumini aliye mwaminifu awe tayari kwenda mbinguni kwa njia ya kumwagwa kwa wingi sana kwa Roho wake. Je! wewe unaionja sasa ile "mvua ya kwanza" katika maisha yako, ambayo inaliandaa kanisa kupokea ile "mvua ya masika" ya Roho? Je! unaishi maisha yaliyojazwa Roho? Ukipewa uwezo huo na Roho, je! utamruhusu Mungu akutumie kupeleka habari ya upendo wake mwingi mno usiosadikika na habari ya kurudi kwake upesi?

7. Masharti Ya Kumpokea Roho Mtaktatifu

Siku ile ya Pentekoste Roho Mtakatifu aliwagusa mioyo wale walioisikia injili hata wakapiga kelele, wakisema, "tutendeje ndugu zetu, tufanye nini sisi?" (Matendo 2:37).

"Petro akawaambia, 'TUBUNI MKABATIZWE, kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo mpate ondoleo la dhambi zenu, NANYI MTAPOKEA KIPAWA CHA ROHO MTAKATIFU" - (Matendo 2:38).

Toba-yaani, kugeuka na kuiacha ile njia ya maisha ya dhambi na kumgeukia Kristo - ndilo sharti la kukipokea kipawa hicho cha Roho [wala sio kwa kunena kwa lugha]. Ili Roho apate kumwagwa juu yetu, ni lazima kwanza tutubu na kumkabidhi Kristo maisha yetu yote. Yesu alikazia pia ule utayari wa kumfuata yeye na kumtii kama sharti jingine la kupokea hicho kipawa cha Roho Mtakatifu (Yohana 14:15-17).

8. Maisha Yaliyojazwa Na Roho

Kabla hajaondoka duniani, Yesu aliwaagiza wafuasi wake, akisema:
"Wasitoke Yerusalemu, bali kingojeeni KIPAWA alichoahidi Baba yangu kuwapa… Kwa kuwa Yohana ALIBATIZA KWA MAJI, bali, ninyi MTABATIZWA KATIKA ROHO MTAKATIFU baada ya siku chache" - Matendo 1:4,5.

Tena na tena Maandiko Matakatifu yanaonyesha kwamba Mkristo hana budi "kujazwa Roho Mtakatifu" (Matendo 2:4; 4:8; 4:31; 6:3; 6:5; 7:55; 9:17; 13:9; 13: 52; 19:6). Roho Mtakatifu anayafanya maisha ya Mkristo kuwa yenye utiifu na mazuri kwa sababu maisha yale yaliyojazwa na Roho hufikia kiwango kile kikamilifu cha maadili ambacho Kristo alikiweka kwa ajili yetu.

Akiwa anaeleza habari za maisha ya Kikristo yaliyojazwa na Roho Paulo alitoa ombi hili kwa niaba ya kila muumini:
"Naomba kwamba kutoka katika utajiri wa utukufu wake AWAFANYE IMARA KWA UWEZA WAKE KWA NJIA YA ROHO WAKE KATIKA UTUKUFU WENU WA NDANI, ili Kristo apate kukaa mioyoni mwenu kwa imani….. Basi, kwake yeye awezaye kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo, KWA KADIRI YA UWEZA WAKE UTENDAO KAZI NDANI YETU."

Kama Frank Moris, aliyekuwa na mbwa wake mwaminifu wa kumwongoza, Basi, sisi tukiwa na kiogozi wetu Roho Mtakatifu ndani yetu, tunaweza kufanya mambo ya ajabu mno kuliko vile tulivyoweza kufanya zamani. Tukiwa na tamaa mpya na uwezo mpya tunawezeshwa naye kusonga mbele kwa imani badala ya kujaribu kuyastahimili tu matatizo ya maisha yetu.

Uzoefu wa kuwa na maisha haya yaliyojazwa na Roho unafanywa kuwa mpya kila siku kwa njia ya maombi na kujivunza Biblia. Maombi yanatusogeza karibu sana na Kristo, na kule kujifunza Neno la Mungu kunatufanya tukaze macho yetu kuelekea kwenye nguvu zake. Mambo hayo yanakivunjilia mbali kizuizi cha aina yote kilichopo kati yetu na Kristo, ambacho kingeweza kumzuia asitumwagie kipawa chake cha Roho, ambacho thamani yake haikadiriki. Hivyo ndivyo tukuavyo na kuziondoa tabia zetu zile mbaya na mielekeo yetu mibaya, na mahali pake kuwekwa tabia nzuri.

Warumi 8 hutoa maelezo ya kusisimua juu ya maisha yaliyojazwa na Roho. Uisome sura hiyo kila uwazapo, na kuzingatia ni mara ngapi Paulo anasonda kidole chake kwa "Roho" wa maisha ya Kikristo.

Je! wewe umefanya ugunduzi wako wa ajabu kuhusu maisha yale yaliyojazwa na Roho? Je! unatambua kuwako kwa huyo Roho katika maisha yako? Je! unauonja ule uweza wake utiao uzima katika maisha yako? Fungua maisha yako ili ule uweza mkuu kuliko wote katika ulimwengu upate kuingia.


© 2004 The Voice of Prophecy Radio Broadcast
Los Angeles, California, U.S.A.