JE! NI MAPEMA KIASI GANI YESU ATARUDI?

Karibu wengi wetu tunao msukumo ambao kwa jumla ni wa kisilika wa kutamani mambo yale yatakayotokea baadaye. Tunataka kujua ni kitu gani kilicho mbele ya upeo wa macho yetu. Lakini utabiri uliosahihi huteleza vibaya sana. Tunao wakati mgumu wa kutosha kuweza kujaribu kubashiri hali ya hewa itakayokuwako kesho!

Lakini yuko Mmoja ambaye unabii wake umethibitika kwamba ni sahihi kwa namna ya kustaajabisha sana. Yesu Kristo, kupitia katika Neno lake, anaweza kutuchukua mpaka siku zile za usoni; yeye ni kiongozi anayetegemewa. Katika somo hili tutaangalia kile alichosema yeye juu ya kuja kwake mara ya pili. Kwa vyo vyote vile, ni nani, basi, ambaye angeweza kujua mengi sana juu ya mwisho wa dunia hii zaidi ya yule aliyeiumba pale mwanzo?

1. Ishara Zionyeshazo Kwamba Kristo Atarudi Katika Siku Zetu

Baada ya Yesu kuwaahidi wanafunzi wake kwamba angekuja tena katika ulimwengu huu kwa mara yake ya pili (Mathayo 23:39), je! ni swali gani walilomwuliza?

"Tuambie,' wakasema, 'mambo hayo yatatokea lini, tena, patakuwa na dalili gani ya kuja kwako, na ya mwisho wa dunia?" - (Mathayo 24:3).

Yesu alijibu waziwazi na pasipo shaka lo lote. Katika sura ya 24 ya Mathayo na sura ya 21 ya Luka yeye mwenyewe aliwapa "ishara" kadhaa, au ushahidi, ambao kwa huo sisi tunaweza kujua kuja kwake kunapokaribia. Unabii mwingine wa Biblia unasaidia kuijazia picha hiyo, unaonyesha kwa kinagaubaga hali ya dunia hii itakavyokuwa kabla tu ya kurudi kwake Kristo.

Kama tutakavyoweza kuona, unabii huo unaendelea kutimia kabisa mbele ya macho yetu; unaonyesha kwamba kuja tena kwa Kristo kumekaribia sana.

Hebu na tuviangalie vibao kumi vya ishara za unabii wa Biblia vilivyo katika njia ile kuu ya kwenda mbinguni, na kuyachunguza maswali ambayo msafiri wa siku hizi anaweza kuuliza anapovisoma vibao hivyo.

Kibao-cha-Ishara ya 1 - Dhiki! Hofu Kuu Mfadhaiko!

Zaidi ya miaka elfu moja na mia tisa iliyopita Yesu alitoa maelezo ya unabii unaohusu maisha ya siku hizi yasikikayo kana kwamba yangeweza kuwa yamechukuliwa kutoka katika habari za jioni hii:
"Tena, kutakuwa na ishara katika jua, na mwezi, na nyota; na katika nchi dhiki ya mataifa wakishangaa kwa uvumi wa bahari na msukosuko wake; watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatayoupata ulimwengu. Kwa kuwa nguvu za mbinguni zitatikisika. Hapo ndipo watakapomwona Mwana wa Adamu akija katika wingu pamoja na nguvu na utukufu mwingi. Basi mambo hayo yaanzapo kutokea changamkeni mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia" - Luka 21:25-28.

Hakuna maelezo yaliyo sahihi zaidi juu ya dunia yetu ya leo kama yalivyo maneno haya: 'Watu watazimia kwa hofu, wakitazamia mambo yatakayoipata dunia hii." Silaha kali zilizolundikana zina uwezo wa kuiteketeza sayari hii yote. Itakuwaje, basi, endapo gaidi mmoja atakipata kichwa kimoja cha nyuklia?

Yesu anatupa sisi msingi wa kuwa na tumaini katika kizazi hiki chenye maafa makubwa. Hali iliyopo sasa ya hatari inayoikabili dunia hii nzima itakayoleta "dhiki na mfadhaiko" inautilia tu nguvu ukweli usemao kwamba kuja kwake Kristo "kunakaribia." Watu siku hizi huomboleza mara kwa mara na kukata tamaa, wakisema, "Tazama ilivyo dunia hii!" Lakini mwanafunzi wa unabii wa Biblia anaweza kusema ghafla kwa sauti iliyojaa matumaini, akisema, "Tazama, NI NANI HUYO ajaye katika dunia yetu."

Kibao-cha-Ishara ya 2: Maafa katika Dunia hii

Je! maafa haya ya asili yanaingiaje na kukubaliana na matukio ya siku za mwisho?
"Kutakuwa na MATETEMEKO makubwa ya nchi, na njaa na TAUNI mahali mahali, na mambo ya kutisha na ishara kuu kutoka mbinguni… Nanyi kadhalika mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba UFALME WA MUNGU U KARIBU" (Luka 21:11,31).

Hebu fikiria habari za njaa kwa dakika moja. Picha za watoto wanaokufa kwa njaa wenye matumbo yaliyovimba huendelea kutangazwa katika habari. Je!hilo si jambo la kushangaza sana kwamba dunia hii inayoweza kuwatuma watu mwezini, HAIWEZI kuwalisha watu wake wote? Yesu alijua kwamba njaa ingeendelea kuwako, kwamba tabia ya uchoyo ya kibinadamu ingezidi kuwa mbaya zaidi na zaidi karibu na ule mwisho wa wakati.

Lakini, je! vipi kuhusu hayo matetemeko ya nchi? Kwa mujibu wa World Almanac ya 1999, karne baada ya karne za kipindi hiki cha kikristo pamekuwa na ongezeko la kustaajabisha la matetemeko makubwa ya nchi: karne ya kumi na nane palikuwa na matetemeko makubwa ya nchi 6; karne ya kumi na tisa yalikuwa 7; karne ya20 yalikuwa zaidi ya 100. Kwa hiyo ushahidi unazidi kuwa wa kuvutia zaidi na zaidi kadiri tunavyokaribia kuzifikia siku hizi zetu.

Takwimu hizo zinauthibitisha unabii ule alioutoa Yesu. Njaa na matetemeko makubwa ya nchi yanazidi kuongezeka taratibu - yakisema, "ufalme wa Mungu umekaribia!" Je! karne yetu hii ya ishirini na moja italeta matetemeko makubwa ya nchi mengi zaidi, au itakuwa ni kuja kwa yule Mfalme wa wafalme?

Kibao-cha-Ishara ya 3: Kujilimbikizia mali.

Hivi maana yake ni nini kwamba utajiri unateleza na kuingia katika mikono ya watu wachache kwa wingi zaidi na zaidi, huku watu wengi zaidi na zaidi wakizidi kuwa maskini?
"Mmejiwekea akiba katika siku za mwisho" - (Yakobo 5:3).

Licha ya ujuzi wetu wote wa uchumi, matajiri wanazidi kuwa matajiri, na maskini wanazidi kuwa maskini. Utajiri wa kuwa na mamilioni mengi ya dola [za Kimarekani] ni kibao-cha-ishara kingine kituonyeshacho kwamba "kuja kwake Bwana kunakaribia" (fungu la 8).

Kibao-cha-Ishara ya 4 - Misukosuko ya Kiraia

Kwa nini hali hii ya kutoridhika na misukosuko miongoni mwa wafanyakazi imeongezeka kwa namna inayojionyesha wazi mno?
"Angalieni! Ujira wa wakulima waliovuna mashamba yenu ninyi mliouzuia kwa hila unapiga kelele dhidi yenu na . VILIO VYAO VYA WALIOVUNA vimeingia masikioni mwa Bwana wa majeshi… Nanyi vumilieni mthibitishe mioyo yenu kwa maana KUJA KWAKE BWANA KUNAKARIBIA" - (Yakobo 5:4,8).

Baada ya kutabiri dhidi ya kujilimbikizia mali nyingi zisizo na idadi katika siku hizi zetu, Yakobo aliona misukosuko ya watu ikitokana na wafanyakazi wasioridhika. Migogoro iliyopo kati ya wale"walio nacho" na wale "wasio nacho" inazidi kuongezeka. Hiyo ni ishara nyingine inayoonyesha kwamba "kuja kwake Bwana kunakaribia."

Kibao-cha-Ishara ya 5: Mmomonyoko wa Maadili

Mbona uzi wa maadili ya jamii unaonekana kana kwamba unakatika vipande vipande?
"Lakini ufahamu neno hili; ya kuwa siku za mwisho kutakuwako na NYAKATI ZA HATARI. Watu watakuwa wakijipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiowatii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasio wapenda wa kwao, wasiotaka suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu - wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake hao nao ujiepushe nao.... LAKINI WATU WABAYA NA WADANGANYAJI WATAENDELEA, NA KUZIDI KUWA WAOVU, wakidanganya na kudanganyika" - (2 Timotheo 3:1-5,13).

Je! kuna mtu ye yote ambaye angeweza kufikiria na kutoa maelezo yaliyo sahihi zaidi ya hayo kuihusu hii dunia yetu? Hebu elekeza kamera yako upande wo wote katika hizi siku tulizo nazo, nawe utapiga picha inayoonyesha ufedhuli utokanao na ile tamaa ya kupenda anasa za ulimwengu huu. Utainasa picha ya kushtua inayoonyesha ukatili wa kuwatenda vibaya watoto wadogo, pamoja na maudhi yanayoletwa kwa makusudi mazima. Utapata matukio mengi yasiyo na idadi ya vijana wasioweza kudhibitika kabisa, pamoja na watoto walio katika ule umri wa miaka ya mwanzo ya ujana wao, yaani, kuanzia miaka kumi na mitatu na kuendelea juu kidogo, ambao wanawaua watu ovyo ovyo na kuwafanya watu vilema. Mambo hayo yote yanajenga chumba kidogo kirefu ambacho kinaonyesha picha zinazotangaza kwa sauti kuu kwamba kuja kwake Yesu kumekaribia sana.

Kibao-cha-Ishara ya 6: Kuenea kwa Dini za Siri (Kiinimacho)

Hivi kwa nini tunauona mlipuko wa kupendezwa sana na dini za siri (occult) miongoni mwa watu?
"Kwa maana watatokea wakristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu [miujiza] wapate kuwapoteza kama yamkini hata walio wateule" -(Mathayo 24:24).

Vifungu hivi vya maneno vinatabiri kwamba wakati huu wa mwisho itaonekana miujiza ya kila namna, pamoja na ishara, yaani maonyesho ya bandia ya uwezo usio wa kawaida kwa wanadamu. Wanawake wachawi na wanaume wachawi wafanyao uchawi wa Kiafrika wataonekana katika maonyesho mbalimbali wakizungumza. Waumini wa Kizazi Kipya (New Age) wako kila mahali, wanauza vijiwe vya uchawi vinavyong'aa kama kioo na maajabu hayo ya uongo hujitokeza ghafla kwa wingi. Hayo yote huyafanya mambo yawe wazi zaidi kama Yesu alivyotabiri kwamba sisi tunaishi katika kipindi cha "kuja kwake Mwana wa Adamu" (fungu la 27.)

Kibao-cha-Ishara ya 7 - Dunia Iliyozinduka

Huko kuzinduka kunakohusu mambo ya dunia hii kunamaanisha nini kwa Afrika, Mashariki ya Kati, Ulaya Mashariki, na kwa matatifa yale ya Mashariki ya Mbali?
"'MATAIFA NA WAJIHIMIZE;… haya utieni mundu, maana mavuno yameiva… kwani uovu wao ni mwingi sana!' Makutano makubwa, makutano makubwa, wamo katika bonde la kukata maneno [kuamua mwisho wa kila mtu]" - (Yoeli 3:12-14).

Leo hii katika nchi za Asia na Afrika, Ulaya Mashariki, Muungano wa Zamani wa Kisovieti, na nchi za Mashariki ya Kati, huenda sisi tunashuhudia kuona mwamko mkubwa sana wa tatifa moja moja katika historia yote iliyopata kuandikwa, "kwa maana siku ya BWANA I KARIBU."

Kibao-cha-Ishara ya 8 - Mipango ya Amani na Maandalizi ya Vita

Tunaishi katika ulimwengu huu wa ajabu. Kila mmoja anaafiki kwamba tungeipatia nafasi amani; lakini basi, zile chuki zilizokandamizwa kwa kipindi cha karne fulani zilizopita, zinalipuka na kuwa vita ya wazi. Nabii Mika na Yoeli walitabiri kwamba wakati ule ule mataifa yatakapokuwa yanasema juu ya shauku yao ya kuwa na amani (Mika 4:1-3) watalazimika kujiandaa kwa vita kutokana na shauku yao waliyo nayo dhidi ya majirani zao (Yoeli 3:9-13).

Zamani sana Biblia ilionyesha picha hii ya mgogoro wetu wa sasa wa kuwa na amani au vita, kisha ikatangaza kwamba amani ya kudumu itatawala katika dunia hii wakati ule tu Yesu atakapokuja.

Kibao-cha-Ishara ya 9 - Maendeleao ya kisasa

Mbona usafiri na mawasiliano vimeuleta ulimwengu huu kuwa karibu mno baada ya karne nyingi za historia ya wanadamu?
"HATA WAKATI WA MWISHO, wengi wataenda mbio huko na huko maarifa yataongezeka" - (Danieli 12:4).

Hapo Danieli anadokeza kwamba maarifa ya kuuelewa unabii wake yataongezeka "katika" (KJV), au "hata wakati wa mwisho." Lakini utabiri huo pia unaonekana kana kwamba unasonda kidole chake kwenye kizazi chetu hiki kilichoyaweka maarifa katika kompyuta. Maarifa ya kila namna yameongezeka kwa kasi kubwa inayolandana na umeme katika miaka hii michache iliyopita. Pamekuwako na mabadiliko mengi sana katika kipindi cha miaka hamsini iliyopita kuliko katika kipindi kile cha miaka elfu mbili kabla yake.

"WENGI WATAENDA HUKU NA KULE kuongeza maarifa." Kabla ya mwaka ule wa 1850, watu walisafiri kwa magari yaliyovutwa na farasi, ikiwa karibu sawa kabisa na vile ilivyokuwa tangu mwanzo wa wakati. Hivi sasa tunasafiri kasi kuliko sauti na kuizunguka dunia hii kwa ndege za konkodi (concorde) hata kwa roketi za safari fupi katika anga za juu.

Ongezeko la safari na gharika ya uvumbuzi ya hivi karibuni hutoa ushahidi mwingine zaidi kuonyesha kwamba sisi tunaishi "katika siku za mwisho."

Kibao- cha- Ishara ya 10 - Injili Ulimwenguni Kote

Yesu alitabiri kwamba, muda mfupi tu kabla ya kuja kwake, injili ingefika katika ulimwengu wote:
"Tena habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote, hapo ndipo ule mwisho utapokuja" - (Mathayo 24:14).

Kwa miongo mingi [makumi mengi ya miaka] karibu nusu ya dunia hii ilikuwa imefungiwa nyuma ya pazia la chuma, ilifungiwa mbali na ile Habari Njema. Lakini baadaye, karibu kwa usiku mmoja Ulaya Mashariki iliteleza kutoka katika kubanwa na chuma cha Ukomunisti. Ukuta wa (Berlin) ukaanguka chini na kuvunjika vipande vipande, na ile dola yenye nguvu nyingi ya Kisovieti ikasambaratika. Ghafla karibu nusu ya sayari hii ilikuwa ikinyoosha mikono yake ili kuipokea injili.

Injili hii inakwenda katika "ulimwengu wote" kwa namna isivyopata kufanyika katika siku zile za nyuma. Kwa njia ya Satelaiti ujumbe wa Kikristo kwa wakati uo huo unaendelea kutangazwa karibu kwa kila taifa. Tunaishi katika kipindi kile kile hasa ambacho Yesu alisema habari zake alipotangaza hivi: "Injili hii itahubiriwa katika ulimwengu wote."

2. Ni Mapema Kiasi Gani Yesu Atakuja?

Baada ya kuyaelezea yale matukio yaliyokusudiwa kuonyesha kipindi kile kinachotangulia muda mfupi tu kabla ya kuja kwake mara ya pili, Yesu anahitimisha maneno yake kwa kusema hivi,
"Amini nawaambia, kizazi hiki hakika hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia " - (Mathayo 24:34).

Hitimisho hilo ni dhahiri - yaani, kizazi hicho kilichodokezwa kwa hivi vibao-vya-ishara za unabii ndicho kitakachojaliwa kumwona Yesu akirudi duniani mara ya pili. Muda hautakuwa mrefu hadi hapo atakapoifagilia mbali dhambi na mateso, na kuusimika ufalme wake ule wa milele. Yesu anatutahadharisha sisi, anasema, "Hakuna aijuaye.. siku ile au saa ile" (fungu la 36.)

Tena, Yesu anaendelea kusema hivi:
"Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja" - (Mathayo 24:44).

3. Yesu, Tumaini Pekee La Dunia Hii

Kristo ndiye tumaini bora la mwisho kwa dunia yetu hii kwa kuwa ni yeye peke yake awezaye kukishughulikia hasa kitu kile kile kinacholivunjilia mbali hilo tumaini - yaani, ile dhambi. Yesu alikufa pale kalwari kufanya uwezekano uwepo wa kuyashinda maovu na kuwapatia ukombozi wale wote wanaoitikia na kuupokea wokovu wake.

"Atendaye dhambi [avunjaye Amri Kumi] ni wa Ibilisi, kwa kuwa Ibilisi amekuwa akitenda dhambi [akizivunja Amri Kumi - Yn. 8:44) tangu mwanzo. Sababu ya kuja kwa Mwana wa Mungu ilikuwa ni kuzivunjilia mbali kazi za Ibilisi" - (1 Yohana 3:8).

Mwokozi wetu alitayarisha njia ya kututoa kutoka katika dunia yetu hii inayovunjika-vunjika kwa kutoa kafara mwili wake na damu yake. Na Yesu yule yule, ambaye siku moja atayaponya magonjwa ya dunia hii kwa kuiteketeza dhambi, hivi sasa anakupa wewe haki yake inayoifutilia mbali hatia ya dhambi katika maisha yako. Huna haja ya kungoja mpaka siku ya kuja kwake mara ya pili ili upate kuwekwa huru mbali na hatia yako na mbali na wasiwasi wako pamoja na ile tabia yako ileayo uharibifu. Yesu yu tayari sana kukupa wewe amani yake katika dakika hii hii.

Mwanamke mmoja kijana alipokuwa akiendelea kuhudhuria katika mikutano ya dini aliguswa moyo wake kiajabu na injili iliyohubiriwa pale. Aliposikia ikifunuliwa habari ya kuja upesi kwa Mwokozi, kila kitu kikaingia vizuri mahali pake. Habari ile ilileta maana kwake. Yeye katika nia yake alikuwa akitafuta upendo, furaha, na amani kutoka kila mahali palikuwa pabaya. Yesu akawa jibu lake.

Siku iliyofuata wakati mwinjilisti yule na mwenzake walipokwenda kumwona, aliwasimulia habari yake yote ya maisha yake machungu na yaliyojaa uhalifu. Alikuwa amezama mpaka chini sana kama mlevi sugu, tena alikuwa akipata riziki yake kwa kufanya umalaya. Baada ya kueleza matatizo yake, alisema hivi huku akilia, "Ulikuwa unanisema mimi hasa jana usiku."

Lakini ile sauti iliyougusa moyo wake ilikuwa ni sauti ya Mungu. Naye alikuwa akisema kwa upole. Aliamua kutoa yote. Alimkaribisha Kristo kuingia moyoni mwake kama Bwana na Mwokozi wake, na kulishikilia sana lile tumaini la kuja kwake upesi.

Katika majuma yale yaliyofuata, akaanza kugundua kwamba zile hofu zake na kutokujisikia salama kwake ambako siku zote alkuwa amejitahidi sana kukuzima kwa kunywa vileo, sasa kulikuwa kumempa nafuu kiasi cha yeye akaanza kumwokoa na kumweka mbali na ile misukumo mibaya iliyokuwa ikimlazimisha kufanya mambo yale mabaya na kuyaharibu maisha yake.

Alikuwa amefanya mambo mengi sana ambayo hakuweza kujivunia. Lakini neema yake Kristo na msamaha wake vilikuwa na nguvu nyingi sana kuliko ile aibu yake. Uzoefu wa maisha aliokuwa nao yule mwizi pale msalabani ulikuwa wa maana sana kwake yule mwanamke. Katika dakika zake zile za mwisho, akitapatapa na kutaka kufa, alimgeukia yule Mteswaji Asiye na Hatia alikuwa kando yake na kumwomba, akasema, "Ee Yesu, unikumbuke mimi utakapokuja katika ufalme wako" (Luka 23:42). Yesu yule yule aliyetoa msamaha wake kwa wingi kwa yule mwizi aliyekuwa akifa, hivi sasa anakupa wewe wokovu, msamaha kamili, na amani moyoni mwako. Hebu leo hii gundua hayo wewe mwenyewe.

Wewe pia unaweza kuomba pamoja na yule mwizi aliyekuwa akifa, na kusema:
"Ee Yesu, unikumbuke mimi utakapokuja katika ufalme wako." Naye Yesu atakujibu hivi, "Nitakuja tena, nawe utakuwa pamoja nami katika Paradiso"


© 2004 The Voice of Prophecy Radio Broadcast
Los Angeles, California, U.S.A.