YESU AJAPO KWA AJILI YAKO

Baada ya miaka mingi ya kutendewa vibaya, Armando Balladares alikuwa amekonda vibaya sana na kulemaa akiwa kama kinyago tu cha vile alivyokuwa mara ya kwanza. Alikuwa amevutiwa sana na imani yake iliyomletea mateso. Muda mfupi baada ya watu wale wawili kuoana katika sherehe ya kuwafungisha ndoa yao iliyoendeshwa kiserikali katika uwanja wa gereza lile, Martha alilazimka kuhamia Miami.

Kutengana kwao kulileta uchungu mwingi sana. Lakini Armando alifanikiwa kutuma kwa siri ahadi yake kwenda kwa mpenzi wake. Juu ya kipande cha karatasi kilichotupwa aliiandika ahadi yake hii:

"Nitakuja kwako. Singe hizo zilizo katika upeo wa mgongo wangu hazitakuwa na maana tena."

Mfungwa huyo alidhamiria kwamba kwa njia fulani yeye na Martha wangetoa ahadi zao ndani ya kanisa mbele za Mungu. Siku moja muungano wao ungekamilika. " Wewe u pamoja nami daima" alimwambia mwanamke yule.

Ahadi aliyotoa Armando ilimfanya aendelee kuishi katika miaka aliyotendewa vibaya sana ambayo ingekuwa imeivunja mioyo ya wanaume wengi. Nayo ilimfanya Martha aendelee kuishi. Alifanya kazi bila kuchoka ili kuyaamsha mawazo ya umma yapate kutambua hali mbaya iliyomkabili mumewe. Yeye hakukata tamaa kamwe.

1. Ahadi

Kuna nyakati fulani sisi tunaweza kujaribiwa na kushangaa, je! hivi kweli siku moja Kristo atashuka na kuja tena katika mbingu hizo za samawi zilizo juu yetu kwa muungano ule wa ajabu pamoja nasi? Mwisho huo wenye furaha wa historia hii ndefu, yenye misiba mingi ya ulimwengu, unaweza kuonekana kama ni mzuri mno kiasi cha kufikiriwa kuwa si wa kweli kwetu sisi. Lakini kuna kitu kimoja ambacho kinaweza kulifanya tumaini letu kuwa hai mioyoni mwetu. Na kitu hicho ni ahadi ya Yesu pekee aliyoitoa kwamba yeye atakuja tena. Muda mfupi tu kabla hajajitenga mbali na wanafunzi wake, Yesu alitoa ahadi hii:
"Yesu aliwaambia, Msifadhaike mioyoni mwenu. Mwaminini Mungu; niaminini na mimi pia. Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama isingekuwa hivyo, ningekwisha waambieni. Sasa nakwenda kuwatayarishieni nafasi. Na nikienda na kuwatayarishieni nafasi, nitarudi na kuwachukueni kwangu, ili nanyi mwe pale nilipo mimi" - (Yohana 14:1-3).

Kabla Yesu hajapaa kwenda mbinguni, aliwaahidi wafuasi wake, akisema "NITAKUJA TENA!" Aliahidi kurudi tena kuja kuwachukua wale wote wanaomtegemea ili awape mahali maalum alipowaandalia. Maandiko yanasema juu ya kuja kwake mara ya pili karibu mara 2,500 hivi. Ukweli kwamba Kristo anakuja mara ya pili katika ulimwengu huu ni wa hakika kama ulivyo uhakika kwamba yeye aliwahi kuishi hapa dunaini miaka elfu mbili iliyopita.

Zamani sana Mungu aliahidi kwamba Masihi angekuja, yaani Mkombozi ambaye angechukua mwilini mwake uovu wetu na kutoa msamaha wake kwa ajili ya dhambi za wanadamu. Ahadi ile ilionekana kana kwamba ilikuwa ni nzuri mno kiasi kwamba isingeweza kuwa ya kweli kwa wengi katika ulimwengu ule wa zamani ambao walikuwa wakiendelea kufanya kazi zao kwa bidii katika maisha yao yote. Lakini kweli Yesu alikuja na kufa juu ya msalaba. Ahadi ilitimia kweli kwa utukufu kuliko vile watu walivyowaza kwamba uwezekano kama ule ungekuwapo. Ahadi yake ya kurudi tena pia itakuwa ni ya kweli. Sisi twaweza kumtegemea yeye atupendaye, kurudi tena na kuwakusanya wale ambao kwa ajili yao amelipa gharama kubwa mno isiyokadirika.

Katika kipindi chote cha kufungwa kwake, Armando aliendelea kutuma kwa Martha kwa siri mashairi, ujumbe, na picha alizochora. Naye [Martha] alifanikiwa kuyachapisha baadhi ya maandiko yale. Ufasaha wake [yale maandiko] uliyavuta mawazo ya ulimwengu. Serikali zikaanza kumbana Castro ili awaachilie wafungwa wale waliofungwa kwa sababu ya kuzifuata dhamiri zao. Rais wa Ufaransa akaingilia kati na hatimaye katika mwezi wa Oktoba mwaka wa 1982 Armando alipakiwa katika ndege iliyokuwa ikienda Paris. Ilikuwa ni vigumu sana kwake kuamini kwamba alikuwa huru-hata wakati ndege ile ilipotua. Lakini basi, baada ya miongo miwili [miaka ishirini] ya mateso na shauku yake ya kungoja, Armando alikimbia na kukumbatiwa na mikono ya Martha.

Miezi michache baadaye katika kanisa la Miami la Mtakatifu Kierani wale wawili wakasimama na kurudia kutoa kiapo chao cha ndoa. Hatimaye muungano wao ukawa umekamilika. Ahadi ikawa imetimizwa: "Nitakuja kwako."

Je, waweza kufikiria ni muungano wa ajabu jinsi gani utakaokuwako hatimaye tutakapoweza kumwona Kristo uso kwa uso? Kuja kwake katika utukufu wake kutazimeza huzuni zetu zote pamoja na kuvunjika mioyo kwetu kote, kutayafutilia mbali maumivu yetu yote tuliyoyaficha mioyoni mwetu. Kurudi tena kwa Yesu kutakidhi shauku zetu zenye kina sana na matarajio yetu ya kusisimua sana. Kisha tutaingia katika umilele wa muungano wa karibu sana na mtu yule wa ajabu sana katika Malimwengu yote. Yesu yu aja upesi! Je, wewe unayo shauku ya kukutana naye?

2. Yesu Atakujaje?

(1) Je! Yesu atakuja kwa siri?
"Tazama, [Yesu] nimekwisha kuwaonya mbele. Basi wakiwaambia, "yuko jangwani,' msitoke; 'yumo nyumbani,' msisadiki. KWA MAANA KAMA VILE UMEME utokavyo mashariki na KUONEKANA hata
magaharibi, HIVYO NDIVYO KUTAKVYOKUWA KUJA KWAKE MWANA WA ADAMU" - (Mathayo 24:25-27).

Umeme unamulika ghafla na kuonekana wazi wazi kabisa mpaka mbali sana, hivyo ndivyo ambavyo kuja kwake Yesu hakutakuwa kwa siri ya aina fulani au kuwa tukio la kihisia tu.

(2) Je, Yesu atakuja tena kama mtu halisi?
"Walipokuwa wakikaza macho mbinguni, yeye alipokuwa akienda zake, tazama watu wawili wakasimama karibu nao, wenye nguo nyeupe, wakasema, enyi watu wa Galilaya mbona mmesimama hapa mkitazama mbinguni? HUYO YESU, aliyechukuliwa kutoka kwenu KWENDA JUU MBINGUNI, ATAKUJA JINSI IYO HIYO mlivyomwona akienda zake mbinguni" - (Matendo 1:10-11).

Siku ya kuondoka kwake kutoka katika dunia yetu hii, malaika wale waliwathibitishia wanafunzi wale kwamba "Yesu yule yule" aliyechukuliwa kwenda mbinguni - si mtu mwingine awaye yote - angerudi tena kama Mfalme wa wafalme. Yesu yule aliyewaponya wagonjwa na kuyafungua macho ya vipofu. Yesu yule yule aliyezungumza kwa upole na mwanamke yule aliyekamatwa akizini. Yesu yule yule aliyeyafuta machozi ya mwombolezaji yule na kuwapokea watoto na kuwakalisha katika paja lake. Yesu yule yule aliyekufa juu ya msalaba ule wa Kalwari akapumzika kaburini, na kufufuka kutoka kwa wafu siku ile ya tatu.

(3) Je, Yesu atakuja ili sisi tuweze kumwona?
"Tazama yuaja na mawingu, na KILA JICHO LITAMWONA" - (Ufunuo 1:7). (Sehemu ya Kwanza).

Wote walio hai wakati Yesu anakuja tena, yaani, wenye haki na waovu, watashuhudia kuyaona marejeo yake. Ni wangapi ambao Yesu mwenyewe alisema watakuona kurudi kwake tena?

"Ndipo itakapoonekana ishara ya Mwana wa Adamu mbinguni, ndipo MATAIFA YOTE YA ULIMWENGU yatakapoomboleza nao, WATAMWONA Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni, pamoja na nguvu na utukufu mwingi" - (Mathayo 24:30).

Kila mtu aliye hai katika dunia yetu hii atamwona Yesu akirudi tena.

(4) Ni nani atakayefuatana na Yesu atakapokuja?
"Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu ule wake" - (Mathayo 25:31).

Fikiria jinsi itakvyokuwa Yesu atakaporudi tena katika fahari yake yote akiwa amezungukwa pande zote na "malaika wote."

(5) Je, tunaweza kutabiri wakati halisi wa kurudi kwake Yesu?
"Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana ila Baba peke yake.... Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja" - (Mathayo 24:36,44).

Kila mmoja atakuona kuja kutukufu kwa Yesu, lakini wengine hawatakuwa tayari kwa kuja kwake huko. Je, wewe binafsi u tayari kwa kuja kwake Yesu?

3. Yesu Atafanya Nini Atakapokuja Tena?

(1) Yesu atawakusanya pamoja wote waliookolewa (wateule).
"Naye atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda, nao watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu" - (Mathayo 24:31).

Kama wewe umemruhusu Yesu akutayarishe moyoni mwako na katika maisha yako, basi utampokea kwa furaha kama Mwokozi. Wako.

(2) Yesu atawaamsha watakatifu waliokufa.
"Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na kwa sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu, nao
WALIOKUFA KATIKA KRISTO WATAFUFULIWA KWANZA" - (1 Wathesalonike 4:16).

Yesu anashuka kutoka mbinguni kwa sauti kuu. Sauti yake yenye nguvu nyingi inasikika ulimwenguni kote. Inayapasua makaburi katika kila eneo la makaburi na kuwafufua mamilioni ya watu waliompokea Yesu katika vizazi vyote. Hiyo itakuwa ni siku ya kusisimua sana jinsi gani!

(3) Yesu atawabadilisha wenye haki wote wakati atakapokuja - si wafu wenye haki peke yao, bali pia wenye haki walio hai.
"Kisha sisi tulio hai, tuliosalia TUTANYAKULIWA PAMOJA NAO katika mawingu ili tumlaki Bwana hewani; Na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele" - (fungu la 17).

Ili kutuandaa sisi kwa maisha yale ya milele, Kristo anabadilisha miili yetu hii inayokufa kuwa miili mizuri isiyokufa.
"Angalieni nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika, kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; Maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika. Maana sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika, nao huu wa kufa uvae kutokufa" - (1 Wakorintho 15:51-53).

Yesu ajapo "sote tutabadilika." Hebu fikiria sasa: hakuna ugonjwa wa baridi yabisi, kupooza, wala kansa. Fungeni hospitali, na fungeni nyumba za matanga. Kristo amekuja!

(4) Yesu atawachukua wenye haki wote kwenda nao mbinguni.
Yesu mwenyewe alitoa ahadi hii, "Nitakuja tena na kuwachukua mpate kuwa pamoja nami" nyumbami mwa Baba yangu (angalia Yohana 14:1-3). Petro anazungumza juu ya urithi wa waliokombolewa "uliotunzwa mbinguni kwa ajili yao" (1 Petro 1:4). Tuanaweza kutazamia mbele kuweza kuyavumbua maajabu ya mji ule wa Mungu, yaani, Yerusalemu Mpya, na kumfahamu Baba yetu aliye mbinguni.

(5) Yesu atayaondoa kabisa maovu na maumivu kwa kipindi chote kitakachofuata.
Waovu - yaani, wale ambao kwa shingo ngumu wameendelea kuikataa rehema yote anayowapa Yesu - wanajihukumu kabisa wenyewe. Wanapokodoa macho yao kutazama uso wa Yesu anapokuja kwao kutoka mawinguni, fahamu zao zinazinduka ghafula na kutambua dhambi zao, tena wanaona ni vigumu kabisa kuvumilia maumivu ya dhambi zao; wanapiga makelele na kuiomba milima na miamba, wakisema, "Tuangukieni, tusitirini mbele za uso wake yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na hasira ya Mwana -Kondoo!" (Ufunuo 6:16). Wanaona ni heri kufa kuliko kusimama mbele za macho ya Yesu yaliyokazwa ambayo yanawaona wote.

Wanajua fika kwamba sauti inayounguruma sasa kutoka mbinguni iliwasihi sana zamani kwa upole ili wapate kuikubali neema ya Mungu. Wale walioamua kupotea wenyewe katika mbio za kiwendawazimu ili kutafuta fedha au anasa au cheo sasa wanatambua kwamba wamekidharau kitu kile cha pekee chenye manufaa ya kweli katika maisha yao.

Ni uvumbuzi unaowamaliza kabisa. Kwa vyovyote vile, hakuna hata mmoja wao ambaye alikuwa na haja ya kupotea. Mungu mwenyewe hakufurahii kufa kwake mtu mwovu" (Ezekieli 33:11). Yeye "hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba" (2 Petro 3:9). Yesu anatusihi sana sisi, anasema, "njoni kwangu ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitwapumzisha" (Mathayo 11:28). Lakini basi, kwa namna isiyosadikika, wengine wanautupilia kando mwaliko huo uliojaa neema.

4. Je! U Tayari Kwa Kuja Kwake Yesu?

Ilimgharimu sana Yesu kutuhakikishia sisi yale maisha mazuri sana ya siku za mbele "nyumbani mwa Baba ya[ke]." Ilimgharimu uhai wake!

KADHALIKA KRISTO NAYE AKIISHA KUTOLEWA SADAKA MARA MOJA azichukue dhambi za watu wengi; Pasipo dhambi kwa hao wamtazamiao kwa wokovu" - (Waebrania 9:28).

Mwokozi yule aliyekufa juu ya msalaba ili kuzichukua dhambi zako, atatokea "mara ya pili" naye atawaletea wokovu wale wanaomngojea." Kristo alijitoa sadaka yeye mwenyewe ili kutupatia sisi wokovu, yaani, kila mmoja wetu. Lakini pasipo kuja kwake mara ya pili, msalaba ule usingefaulu kutokana na kazi yake aliyoifanya. Kristo anataka kutupatia sisi makao salama pamoja naye milele zote. Ili jambo hili lipate kutimizwa, yatupasa sisi kumruhusu yeye ili atawale ndani ya mioyo yetu kama Mwokozi na Bwana wetu kuanzia hivi sasa.

Alfajiri moja ya tarehe 16, Agosti, 1945 mvulana mdogo alikimbia kupitia katika kiwanja cha Shantung katika China ya kaskazini, akipiga makelele na kusema kwamba ameiona ndege angani. Wafungwa wote wenye miili yenye nguvu wakakimbia na kutoka nje na kutazama juu. Wanaume hao pamoja na wanawake walikuwa wameteseka sana kwa miaka mingi ya kukaa upweke, umaskini, na wasiwasi, wakiwa wamefungwa na Wajapani kama raia wa mataifa yale ya kiadui. Kwa wengi wao kitu kimoja tu kilikuwa kimewafanya kuwa hai kiroho: tumaini kwamba siku moja vita ile ingekoma.

Mshtuko kama wa umeme vile ukaenea katika lile kundi la wafungwa 1500 waliokuwa wangali hai walipotambua kwamba ndege ile ilikuwa inakuja kwa ajili yao. Mlio wa ndege ile ulivyozidi kuwa mkubwa zaidi na zaidi, mtu fulani mmoja akapiga kelele, akasema" Tazama, ile ni BENDERA YA KIMAREKANI imechorwa pembeni kwa rangi!" Nao wakiwa wamepigwa na bumbuazi kwa kutokuamini kwao, sauti zikapiga makelele, "Tazama, WANATUPUNGIA mikono! Wanajua sisi ni akina nani. Wanakuja kutuchukua."

Kwa wakati huo ulikuwa ni zaidi ya vile walivyoweza kumudu kuuzuia watu wale waliovaa nguo zenye viraka, waliokuwa wamechoka sana, na wenye shauku ya kurudi nyumbani kwao ambao walikuwa wameendelea kuwa hai. Vurumai ikazagaa pote. Watu walikuwa wakikimbia katika miduara, wakipiga makelele yao kwa nguvu zao zote, wakipunga hewani mikono yao na kulia.

Ghafla kundi lile likaanza kuhema kwa mshangao na kukodoa macho kimya kimya. Sehemu ya chini ya ndege ikafunguka ghafla na watu wakaanza kuelea angani wakishuka chini kwa miavuli. Waokoaji wao walikuwa hawaji tu siku fulani moja ya baadaye; walikuwa wanakuja leo, SASA HIVI ili kuwa miongoni mwao!

Kundi lile likasonga mbele kuelekea kwenye lango la uwanja ule. Hakuna aliyesimama na kuwaza juu ya zile bunduki za rashasha zile zilizokuwa zimeelekezwa chini kwao kutoka kwenye minara ile. Baada ya miaka mingi ya kukata tamaa na upweke, wakalivunja lile lango na kutimua mbio kuelekea mahali kule walikokuwa wakitua wale askari wa miavuli.

Punde si punde gharika ya wanadamu ikarudi na kuingia kwa wingi ndani ya kambi ile - wakiwabeba wale askari mabegani mwao. Mkuu wa kambi akasalimu amri bila kupigana. Vita vilikuwa vimekwisha kweli. Uhuru ulikuwa umekuja. Ulimwengu uligeuka na kuwa mpya kabisa tena.

Upesi Mungu WETU, yaani, Mwokozi WETU, atashuka kutoka mawinguni kuja kutuokoa sisi. Kisa hiki cha kuogofya sana cha muda mrefu sana cha ukatili wa mwanadamu kwa mwanadamu mwenzake hatimaye kitakoma kabisa. Patakuwa na shangwe kuu siku ile, makelele ya furaha hatimaye tutakapojua kwamba: "Anakuja karibu sana nasi; naweza kuwaona malaika wakizipiga zile tarumbeta zao." Sauti inazidi kuwa kubwa zaidi, wingu lile lenye utukufu linazidi kung'aa zaidi na zaidi, mpaka sisi tunashindwa kustahimili kuliangalia. Lakini basi, sisi hatuwezi kuacha kuliangalia tunapotambua kwamba: "Yeye ananiona mimi! Anajua mimi ni nani." Tukiwa tumejaa furaha isiyoelezeka tutajua, tutasema: "huyu ndiye Mungu wangu. Anakuja kwa ajili yangu, sio siku fulani ya baadaye, bali leo, sasa hivi."

Je, wewe uko tayari kumpokea huyo mfalme (mtawala) katika utukufu wake wote kama siyo, basi, tafadhali mwalike Yesu wewe mwenyewe ili aingie ndani ya maisha yako sasa hivi. Kama vile kuja kwa Yesu katika dunia yetu hii kutakavyoyatatua matatizo ya ulimwengu huu, ndivyo kuja kwake ndani ya moyo wako kutakavyokusaidia wewe kushughulika na matatizo yako ya sasa ya kila siku. Mtatuaji mkuu wa matatizo anaweza kukuokoa wewe kutokana na hatia na mzigo wako wa dhambi na kukupa wewe uzima wa milele.

Kuja kwa Yesu katika maisha ya mtu kunaweza kuyabadilisha milele kwa namna ya kuvutia sana kama kuja kwa Yesu kutakavyoibadilisha kabisa. Unaweza kumtegemea Yesu. Atakutayarisha wewe kwa ajili ya kuja kwake na kukupa ahadi ya ajabu ya maisha yale ya milele yenye furaha.


© 2004 The Voice of Prophecy Radio Broadcast
Los Angeles, California, U.S.A.