NAFASI YA PILI YA KATIKA MAISHA

Baada ya kuishi karibu maisha yake yote kama mfuasi wa Budha, mtu wa makamo mmoja katika nchi ya Singapore aliyekuwa amegeuka na kuwa Mkristo aliulizwa swali hili, "Bwana Limu, je, wewe unaona tofauti gani kati ya kuwa mfuasi wa Budha na kuwa Mkristo?

"Hilo ni rahisi," alijibu. "Tangu mimi nimempokea Yesu kama Mwokozi wangu, nina amani nyingi ajabu moyoni mwangu."

Hilo ndilo linalotokea tunapoyaweka maisha yetu ndani ya Kristo.

"Wewe [Mungu] utamlinda katika amani kamilifu, yeye ambaye moyo wake umekutegemea, kwa kuwa anakutumaini" - (Isaya 26:3).

Kuishi maisha ya Kikristo huleta amani kamilifu - hisia kamili ya kuwa na usalama na raha.

Wale walioligundua hili wameiona njia pekee ya kupata nafasi ya pili ya kuishi - yaani, kumpata Yesu!

1. Maana Ya Kupotea

Yawezekana kwa mtu aliye hai kimwili kuwa na kile watu wengine wanachokiita kustarehe, na bado akawa amekufa - yaani, amekufa kiroho.

"NANYI MLIKUWA WAFU KATIKA MAKOSA NA DHAMBI ZENU, ambazo mlizoziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga roho YULE [MWOVU] ATENDAYE KAZI SASA katika wana wa kuasi" - Waefeso 2:1,2.

Shetani anamwongoza mtu yule aliyekufa kiroho na kushuka naye kuelekea chini ya ngazi ya dhambi na kutotii. Lakini kweli ile ya ajabu ya injili inasema kwamba Mungu anawapenda watu kama hao. Anawapenda wakiwa wamekufa katika dhambi zao, kisha anawapa ukombozi kamili na wa bure [bila gharama] kutoka katika hatari yao.

"Lakini Mungu ni mwenye huruma nyingi. Alitupenda kwa pendo lisilopimika, hata, ingawa tulikuwa tumekufa kwa sababu ya dhambi, alitufanya hai pamoja na Kristo. Kwa neema ya Mungu ninyi mmeokolewa. Kwa kuungana na Kristo Yesu, Mungu alitufufua pamoja naye, tukatawale pamoja naye mbinguni. Ndivyo alivyopenda kuonyesha kwa watu wa nyakati za baadaye ukuu wa neema yake aliyotujalia kwa ukarimu katika kuungana kwetu na Kristo Yesu" - (Waefeso 2:2-7).

Mungu alitupenda sisi tulipokuwa hatuna cha kupendeka ndani yetu. Neema yake iliweka ndani yetu maisha mapya ndani ya Kristo. Hatuwezi kujibadilia wenyewe, ila Mungu anaweza. Tunapokuja kwake kwa imani na unyenyekevu, anatupa nafasi ya pili ya kuishi kama zawadi inayotolewa bure.

2. Ni Kutoka Katika Nini Tunahitaji Kuokolewa?

(1) Twahitaji kuokolewa kutoka katika dhambi.
"Wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu" - (Warumi 3:23).

Kusema bila kuficha: sisi hatuishi kulingana na kile tunachojua kuwa ni haki. Mzazi akisongwa sana na matatizo hasira yake inaweza kulipuka na kumwumiza kihisia mtoto wake. Mtu fulani anaweza kumkasirikia sana dereva mwingine na kuwa karibu sana kusababisha ajali. Mwanafunzi anaweza kuchukia na kusema maneno mabaya kwa kunong'ona dhidi ya mwanafunzi mwingine. Mfanya biashara anaweza kupanga "kusahau" chanzo fulani cha mapato yake wakati wa kutozwa kodi. "Wote wamefanya dhambi", hiyo ndiyo hali ya wanadamu.

Biblia inaelezaje maana ya dhambi?
"Kila lisilo la haki ni dhambi" - (1Yohana 5:17).

Tunahitaji kuokolewa kutoka katika aina zote za tabia zetu mbaya pamoja na misukumo ya ndani inayotushurutisha kufanya mambo fulani mabaya: kama vile, kusema uongo, hasira inayomfanya mtu atukane watu, tamaa mbaya za mwili, uchungu, kutaja machache tu.

"Kila atendaye dhambi afanya uasi kwa kuwa dhambi ni uasi" (1 Yohana 3:4).

Kwa ajili hiyo, sisi tunahitaji kuokolewa kutoka katika dhambi - yaani, kutoka katika uvunjaji amri [kumi] za Mungu.

(2) Twahitaji kuokolewa kutoka katika uhusiano wetu na Mungu ambao ulivunjika.
"Lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu; na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone" - (Isaya 59:2).

Dhambi ile isiyosamehewa inakata uhusiano wetu na Mungu. Kristo alikuja kuturudishia tumaini letu kwa Mungu, ambalo Shetani alikuwa amelidhoofisha.

(3) Twahitaji kuokolewa kutoka katika mauti ya milele. - adhabu ya dhambi [kuvunja amri Kumi].
"Kwa hiyo kama mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti, na kwa hivyo mauti ikawafikia watu wote, kwa sababu wote wamefanya dhambi" - (Warumi 5:12).

(4) Twahitaji kuokolewa kutoka katika maisha yetu ya dhambi yasiyo na furaha, yaliyo tupu.

Kwa mwenye dhambi, maisha ni kama mtaa uliofungwa mwisho wake.

(5) Twahitaji kuokolewa kutoka katika ulimwengu wenye dhambi.

Ni lazima tuokolewe kutoka katika ulimwengu uliojaa dhambi na athari zake - kama vile, umasikini, huzuni kubwa moyoni, upweke vita, magonjwa na kifo!

3. Ni Nani Awezaye Kutuokoa?

Yesu peke yake aweza kutuokoa sisi.
(1) Yesu aweza kutuokoa sisi kutoka dhambini.
"Naye atazaa mwana nawe utamwita jina lake Yesu, maana yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao" - (Mathayo 1:21).

Baniani [Mhindu] mmoja alimwambia rafiki yake Mkristo maneno haya, "Mimi napata mambo mengi katika dini hii ya Kihindu ambayo hayapatikani katika Ukristo, lakini kuna kitu kimoja Ukristo ulicho nacho ambacho dini ya Kibaniani haina - yaani, Mwokozi." Ukristo ndiyo dini pekee katika ulimwengu huu inayowapa watu Mwokozi.

(2) Yesu anaweza kutuokoa kutoka katika uhusiano wetu na Mungu ambao ulivunjika.
"Mlitengwa mbali na Kristo... mlikuwa hamna tumaini, wala hamna Mungu duniani. Lakini sasa katika Kristo Yesu ninyi ambao zamani mlikuwa mbali, mmeletwa karibu kwa damu yake Kristo" - (Waefeso 2:12,13).

Yesu ndiye Rafiki mkamilifu ambaye twaweza kufurahia kuwa na uhusiano naye. Yeye anapenda kijitokeze ndani yetu kile kilicho bora sana. "Kwa damu yake Kristo" maisha yetu ya dhambi yaliyopita yanasamehewa, na siku-kwa-siku yeye anatupa ukubali wake, nguvu za kushinda dhambi, na maisha yake makamilifu. Tunajua kwamba atakuwa pale kutuinua na kila wakati tunapoanguka. Kwa upande wetu upendo wetu kwake unazaa shauku ya kuishi kwa kufuata njia ile impendezayo yeye.

(3) Yesu anaweza kutuokoa sisi kutoka katika ile mauti ya milele, adhabu ya dhambi.
"Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti [ya milele]; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu" - (Warumi 6:23).

Sisi tu wavunjaji wa sheria yake [amri za Kumi], tumehukumiwa kufa. Yesu anatuokoa sisi kutoka katika mauti ya milele, kisha anatupa uzima wake wa milele.

"Mungu auonyesha dhahiri upendo wake kwetu sisi; tulipokuwa tungali wenye dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu" - (Warumi 5:8).

Kwa sababu ya upendo wake usio na mwisho, Yesu "alikufa kwa ajili yetu na kupata mateso kamili ya dhambi zetu, Mungu sasa anaweza kuwasamehe na kuwakubali wenye dhambi bila kuihafifisha hiyo dhambi.

(4) Yesu anaweza kutuokoa kutoka katika maisha ya dhambi, yasiyokuwa na furaha.
"Hata imekuwa mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya - ya kale yamepita, tazama! Yamekuwa mapya"- (2 Wakorintho 5:17, Philips).

Hatuwezi kujiokoa wenyewe kutoka katika dhambi au kuigeuza tabia yetu kwa kujitegemea wenyewe kama vile Simba asivyoweza kuamua awe mwana-kondoo (Warumi 7:18). Dhambi ina nguvu nyingi kuliko nia yetu ya kufanya yale tuyatakayo. Lakini Kristo anaweza kukufanya wewe uwe "imara kwa uweza wake, kwa kazi ya Roho wake katika utu [wako] wa ndani" (Waefeso 3:16). Anafanya kazi yake ili kuondoa tabia zetu ziletazo uharibifu na mahali pake kuweka tabia hizi nzuri: upendo, amani, furaha, upole, uwezo wa kujitawala (Wagalatia 5:22,23). Kristo anaishi maisha yake kupitia ndani yetu, kisha tunapokea uponyaji wa kiroho, tunarejeshwa katika maisha mapya, na kuwezeshwa kuishi maisha hayo mapya.

Harold Hughes alikuwa amepoteza tumaini lake kabisa la kuweza kubadilika kwa wakati uwao wote ule. Alikuwa amejitahidi sana kuacha kunywa pombe mara nyingi sana. Alijua fika kwamba vita yake dhidi ya chupa ya pombe ilikuwa imewaletea maisha ya jehanamu mke wake na binti zake wawili kwa miaka kumi kamili. Basi asubuhi moja yenye baridi kali akaingia katika bafu lake na kuuelekeza mtutu wa bunduki yake kinywani mwake. Kabla hajafyatua risasi, aliamua kwamba ingekuwa heri kwake kumweleza Mungu mambo yake yalivyokuwa. Sala yake ile ikageuka na kumfanya alielewa kwikwi kwa muda mrefu akimsihi amsaidie.

Mungu akamjibu. Harold Hughes akajitoa kabisa kwa Kristo na kupata nguvu za kiroho kumwezesha kulishikilia lile tumaini lake la kubadilika. Aliacha kabisa kunywa pombe, akawa mume na baba mwenye mapenzi na wa kutegemewa, kisha akasonga mbele na kujipatia kiti katika Seneti [sehemu ya Bunge] la Marekani. Harold Hughes aligundua uwezo mkubwa kabisa unaoyabadilisha maisha ya watu katika dunia hii - yaani, Yesu!

(5) Yesu anaweza kutuokoa kutoka katika dunia hii ya dhambi.
Miongozo minne ya GUNDUA ifuatayo itaeleza jinsi jambo hilo linavyoweza kufanyika.

4. Tunaokolewa Kwa Kuchukua Hatua Rahisi Tatu

Hatua ya 1. mwombe Kristo aingie na kuishughulikia dhambi katika maisha yako.
Je, sisi tunayo sehemu gani ya kufanya ili kuondokana na maisha yetu haya ya dhambi?

TUBUNI, basi na kumgeukia Mungu, ili dhambi zenu zipate kufutwa kabisa"
- (Matendo 2:38).

Ni kitu gani kinachomwongoza mtu kutubu?
"WEMA WA MUNGU WAKUVUTA WEWE UPATE KUTUBU" - (Warumi 2:4).
"HUZUNI YENU ILIWAONGOZA HATA MKATUBU" - (2 Wakorintho 7:9).

Toba ni kuhuzunika tu kwa ajili ya maisha yetu ya dhambi yaliyopita, kisha kugeuka na kwenda mbali na dhambi zetu, tukizikomesha tabia zetu mbaya za zamani, pamoja na mazoea yetu, na mtazamo wetu. Hivyo si huzuni kwa sababu sisi tunaogopa tu ile adhabu, bali ni mwitikio wetu kwa ule "wema wa Mungu" uliomfanya Yesu kufa badala yetu kwa ajili ya dhambi zetu. Tunaikataa dhambi kwa sababu inamwumiza Mungu.

Tunapoyaonja maisha mapya ndani ya Kristo, tungeyasahihisha makosa yetu tuliyofanya zamani kwa kadiri iwezekanavyo (Ezekieli 33:14-16).

Je, sehemu ya Mungu ni ipi katika kutuondolea maisha yetu yenye dhambi ya zamani?

Mambo yote mawili, toba na msamaha, ni vipawa vitokavyo kwa Mungu.
"Mungu amemtukuza kwa kumweka mkono wake wa kulia, awe mkuu na Mwokozi ili apate KUWAPA TOBA na MSAMAHA WA DHAMBI" - (Matendo 5:31).

Nasi tunapotubu, Mwokozi huyo mwenye upendo anatusamehe dhambi zetu, anatusafisha dhambi zetu, na kuzitupa katika vilindi vya bahari.
"TUKIZIUNGAMA dhambi zetu, YEYE NI MWAMINIFU na wa haki, NAYE ATATUSAMEHE dhambi zetu na KUTUSAFISHA na udhalimu wote" - (1 Yohana 1:9. Angalia pia Mika 7:18,19).

Hakuna dhambi ambayo ni ya kutisha sana asiyoweza kuisamehe Mwokozi wetu aliyekufa kwa sababu ya hizo dhambi zetu juu ya msalaba ule wa Kalvari. Mtu yule anayemtumainia Yesu anahitaji tu kumwomba yeye ili ampe msamaha wake. Kufa kwake Kristo kwa ajili yetu hakuwezi kutupatia sisi msamaha mpaka tuombe kusamehewa. Ni ukweli ulio na busara ndani yake ya kwamba dhambi zetu zilichangia katika kuipigilia ile misumari na kutoboa viganja na nyayo zake Kristo. Na, hata hivyo, Yesu anayo shauku nyingi sana kuliko vile tuwezavyo kuwaza ili tupate kukipokea kipawa chake cha msamaha na upatanisho.

Habari zilimfikia kijana mmoja mwanaume aliyekuwa ametoroka nyumbani kwao kwamba mama yake alikuwa akifa. Habari zile zikamjaza majuto mengi kuhusu uhusiano wao uliokuwa umevunjika. Akaharakisha kwenda nyumbani, akaingia haraka katika chumba kile na kujitupa juu ya kitanda cha mama yake. Machozi yakiwa yanabubujika akamsihi amsamehe.

Akamvuta karibu na kunong'ona, "Mwanangu, ningekuwa nimekusamehe zamani sana endapo ungekuwa tu umeniomba mimi."
"Kama wewe umetanga mbali na Mungu - au bado hujamjua - tafadhali fikiria jinsi Baba yako, akupendaye, aliye mbinguni alivyo na shauku kubwa kukukaribisha nyumbani kwake. Zaidi ya kitu kinginecho chote yeye anataka wewe upokee msamaha wake anaokupa. Yesu anakupenda wewe. Alikufa kwa ajili yako. Siku zote yu tayari kukusamehe wewe. Basi itikia mwaliko wake wa neema unaokutaka utubu. Ungama dhambi zako. Amini naye anafanya hivyo. Mtumainie yeye! Tegemea ahadi zake.

Hatua ya 2. pokea maisha mapya toka kwa Yesu.
Sehemu yako katika kupokea maisha mapya toka kwa Yesu ni kuamini kwamba Yesu amekuokoa kweli kweli. Kubali bila swali ukweli kwamba yeye amekusamehe na kukusafisha, ameyaondoa maisha yako ya dhambi ya zamani, na kukupa wewe maisha mapya kabisa yaliobadilika.
"Bali wote... waliompokea, aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu" - (Yohana 1:12).

Wewe kama mtoto wa Mungu, unayo "haki" ya kupokea hayo maisha mapya kutoka kwa Yesu. Kama tulivyokwisha kusema, wewe huwezi kuipata hiyo kwa kujitegemea mwenyewe - ni zawadi toka kwa baba yako aliye mbinguni! Yesu anatoa ahadi kama hiyo iliyo ya kweli ili kutuondolea wasi wasi na mashaka yetu.

Je, sehemu ya Mungu ni ipi katika kutupa sisi maisha hayo mapya?
"Yesu akamwambia, Amini, amini nakuambia, hakuna mtu awezaye kuuona ufalme wa Mungu asipozaliwa mara ya pili" - (Yohana 3:3).

Kulingana na Yesu, mwenye dhambi aaminiye na kutubu, anazaliwa kabisa na kuwa na maisha mapya. Ni mwujiza ambao ni Mungu peke yake awezaye kuufanya. Yeye anaahidi hivi:
"Nami nitawapa ninyi MOYO MPYA, nami nitatia ROHO MPYA ndani yenu; nami nitatoa moyo wa jiwe uliomo ndani yenu, nami nitawapa moyo wa nyama"- (Ezekieli 36:26).

Yesu anaubadilisha moyo wetu - yaani, hisia zetu pamoja na tabia zetu - kisha anakaa "ndani yetu" (Wakolosai 1:27). Maisha hayo mapya si wazo moja tu lililo zuri la kiroho; ni ukweli ulio mkakamavu na imara, ni ufufuo kutoka katika kifo cha kiroho kwenda katika maisha hayo mapya kabisa na uzima.

Hatua ya 3. Uishi kwa ajili ya Kristo kila siku.
Maisha ya Kikristo yanamaanisha kugeuka kila siku kutoka katika kujipenda wenyewe na kuingia katika kifungo na Yesu atupendaye. Tunakua katika maisha hayo mapya kwa kuuimarisha uhusiano wetu na Yesu. Hii ina maana kwamba wakati wetu bora tuutumie pamoja naye, tukijenga mawasiliano ya kweli na yaliyo wazi. Mungu ametupa sisi misaada mitano kwa ajili ya kukua kwetu kiroho: Kujifunza Biblia, maombi, kutafakari, kuwa na ushirika pamoja na Wakristo wengine, na kubadilishana uzoefu wetu wa maisha na wengine.

Kuishi ndani ya Kristo hakuna maana kwamba hatuwezi kamwe kufanya makosa. Lakini tunapojikwaa na kutenda dhambi, tunadai msamaha wake Kristo, kisha tunasonga mbele. Tuanaelekea upande fulani, tena tunajua kwamba Kristo, anaendelea kuishi ndani ya mioyo yetu.

Jinsi Tupokeavyo Maisha Mapya Toka Kwa Kristo
1. Tunamwamini yeye na kumpokea kama Mwokozi na Bwana wetu.
2. Tunajenga uhusiano wetu pamoja nao. (kuwa na muda fulani kila siku wa maombi na kusoma Biblia ni jambo la muhimu sana.)
3. Kristo hufanya kazi yake kwa njia ya Roho wake Mtakatifu ili kuziondoa tabia zetu mbaya na kuziweka tabia zake nzuri mahali pake.

5. Furaha Ya Kupewa Nafasi Hiyo Ya Pili

Harold Hughes alipewa vyeo vingi katika kazi yake maarufu kama seneta wa Marekani, lakini kimoja cha maana sana kwake kilikuja muda mfupi tu baada ya kujitoa kwake kwa Kristo.

Jioni moja Harold alikuwa akijifunza Biblia yake akiwa peke yake katika sebule yake alipoguswa na kiwiko kwenye kiwiko chake. Akaangalia juu. Walikuwa ni wale binti zake wadogo wawili, wakiwa wamesimama kimya katika magauni yao ya kulalia usiku. Akawakazia macho kwa dakika moja hivi; walikuwa wamebadilika sana, naye alikuwa amekosa mengi wakati ule alipokuwa akipambana vita dhidi ya chupa ya pombe iliyokuwa ikimletea uharibifu.

Hapo ndipo Carol, mdogo zaidi, aliposema, "baba, tumekuja kukubusu na kukutakia usiku mwema."

Macho ya yule baba yakaingiwa na kiwi muda mrefu mno ulikuwa umepita tangu watoto wale walipokuja kwake na kukumbatiwa naye. Sasa yale macho yao mazuri na maangavu hayakuwa na hofu yo yote. Hatimaye baba yao alikuwa amekuja nyumbani.

Yesu anawapa watu wake nafasi ya pili kweli. Anawachukua wale walio wabaya kupindukia na kuwapa mianzo mipya.

Mwokozi anatamani sana kwamba kila mmoja wetu hatimaye arudi nyumbani. Je, umeukubali huo mwaliko wa upendo wa Kristo anaotoa kwako? Kupokea msamaha na utakaso wa Mungu ni jambo rahisi na la maana sana kama kuinyosha mikono yako na kumkumbatia mtoto ndogo.

Iwapo wewe bado hujamtumainia Kristo kama Mwokozi wako binafsi, basi, unaweza kufanya hivyo sasa hivi kwa kutoa ombi kama hili:
"Baba, nasikitika kwa ajili ya maisha yangu ya dhambi ya zamani. Asante kwa kumtuma Mwanao katika dunia hii kuja kufa badala yangu mimi. Yesu, tafadahli nisamehe dhambi zangu na kuingia katika maisha yangu na kuniokoa. Nataka nipewe nafasi ya pili ya kuishi maisha yangu - nataka kuzaliwa mara ya pili. Naam, zaidi sana, nataka kujenga uhusiano wangu siku-kwa-siku pamoja nawe. Asante kwa kunifanyia mwujiza huo ndani yangu. Katika jina la Yesu, Amina."

Fanya ugunduzi huu wa ajabu: sisi tunapokuja kwake, Yesu hufanya kazi yake ya kutuokoa.


© 2004 The Voice of Prophecy Radio Broadcast
Los Angeles, California, U.S.A.