DARAJA KWENDA KWENYE MAISHA YANAYORIDHISHA

Waliikuta mifupa yake kando ya kibanda chake cha muda katika kisiwa kisichokuwa na watu katikati ya Atlantiki. Baharia yule asiyejulikana jina lake alitunza kitabu cha mambo ya kila siku kilichoeleza kwa kinagaubaga mateso mabaya aliyopata kwa miezi minne. Alikuwa ametelekezwa pwani ya kisiwa cha Ascension na kundi la manowari za Kiholanzi chini ya kamanda mmoja katika mwaka wa 1725 kwa uhalifu wake fulani uliokuwa haujatajwa. Baada ya muda mfupi kupita, akawa akinywa damu ya kasa ili kuituliza kiu yake kali sana. Mateso ya mtu yule kimwili yalikuwa makali sana, lakini maumivu makubwa zaidi yanaonekana wazi katika kitabu chake cha mambo ya kila siku: yaani, ile hatia yake iliyomlemea kabisa.

Aliandika maneno yaliyomtesa sana kama haya: "Ni maumivu yaliyoje yanayowapata wanadamu wanaoziacha njia za haki, wakifurahia kuongeza idadi ya watu waliolaaniwa." Kutengwa kabisa kwa baharia yule katika kisiwa kile cha upweke kulitokana na hisia yake ya kutengwa mbali na Mungu. Hilo ndilo jambo ambalo mwishowe lilionekana kwake kuwa halivumiliki.

Wanadamu wamekuwa wakipambana na kutengwa huko mioyoni mwao tangu Adamu na Hawa walipo"jificha BWANA Mungu asiwaone kati ya miti ya bustani" baada ya kula lile tunda lililokatazwa (Mwanzo 3:8). Hisia mpya, ngeni, za kuona aibu, hatia, na hofu zikawalazimisha wale watu wawili, mume na mke, kumkimbia Mungu alipokuja na kuwaita. Hisia zile, kwa bahati mbaya, sasa zinafahamika sana kwetu.

Je, ni kitu gani kinachosababisha utengo huo kati yetu na Mungu?
"Lakini maovu yenu yamewafarakisha ninyi na Mungu wenu; dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone" - Isaya 59:2.

Ufa huo mkubwa unaowatenga wenye dhambi mbali na Mungu hautokani na Mungu. Mungu hakutimua mbio kumwacha Adamu na Hawa - wao ndio waliomkimbia yeye.

1. Kukidhi Njaa Yetu Iliyojificha

Kabla dhambi haijaiharibu ile picha, Adamu na Hawa waliufurahia urafiki wao wa karibu sana na Muumbaji wao katika makazi yao yale katika ile Bustani nzuri ya Edeni. Kwa bahati mbaya sana, waliukubali ule uongo wa Shetani kuhusu jinsi ambayo wao wangekuwa na hekima kama Mungu, wakakivunja kile kifungo cha imani kilichokuwapo kati yao na Muumbaji wao (Mwanzo 3).

Baada ya kufukuzwa katika ile Bustani ya Edeni, Adamu na Hawa waliona maisha yao yakizidi kuwa magumu sana kule nje. Kuzaa watoto na kuilima ardhi sasa kukawa ni kwa kutokwa na damu, jasho, na machozi. Uhusiano wao wa karibu sana na Mungu ukavunjika, wakajikuta hawana kinga yo yote dhidi ya tamaa zao zisizotoshelezeka na shauku zao ziwaleteazo maumivu makali - yaani, huo upweke uletwao na dhambi.

Tangu Adamu na Hawa walipotenda tendo lao la uasi la kwanza, "wote" (jamii yote ya mwanadamu) wameanguka na kuwa na mwelekeo ule ule mmoja wa dhambi na kukabiliwa na kifo, yaani, hiyo ndiyo adhabu ya mwisho ya dhambi.
"Kwa hiyo, kama vile dhambi ilivyoingia ulimwenguni kupitia kwa mtu mmoja, na mauti kwa njia ya dhambi hiyo, na hivyo MAUTI IKAWAFIKIA WATU WOTE, kwa sababu WOTE WAMEFANYA DHAMBI" - (Warumi 5:12).

Sisi sote tunaona njaa kubwa moyoni mwetu kwa kile tulichokwisha kukipoteza, yaani, tunakuwa na shauku ya kupata usalama wa aina fulani ambao ni Mungu tu awezaye kutupa. Mara kwa mara sisi tunajitahidi kuikidhi hiyo njaa kwa kuwa walevi wa kununua vitu madukani, au kuwa na mbio za wendawazimu za kutaka kupandishwa cheo kazini, au kwa kuizimisha tu hiyo njaa kwa kutumia alkoholi [pombe], madawa ya kulevya au kwa uzinzi.

Lakini hizo shauku zetu zote ni dalili ya upweke wa kutokuwa na Mungu. Wala hakuna tiba isipokuwa kwa kuuonja upendo wake katika maisha yetu.

"Utanijulisha njia ya uzima, mbele za uso wako ziko furaha tele. Na katika mkono wako wa kuume. Mna neema milele" - (Zaburi 16:11).

Kuridhika kweli kweli huja tu kama ufa ule uliopo kati yetu na Mungu umejengewa daraja, na sisi tunaweza kuvuka ng'ambo na kuingia mbele zake.

2. Kuziba Ufa Wa Dhambi Na Mauti

Wanadamu sio pekee yao tu wafanywao kuwa wakiwa kutokana na dhambi hiyo. Moyo wa Mungu pia uliumia sana siku ile Adamu na Hawa walipomgeuzia migongo yao. Na bado yeye anaendelea kusikitika kuhusu ile huzuni na misiba inayowapata wanadamu. Mungu anatamani sana kukidhi tamaa zetu zilizojificha na kutuponya majeraha yetu ya kimaadili. Hakuwa ametosheka kuangalia kwa huruma ng'ambo ya ufa ule uanaotutenga sisi mbali naye. Mungu akaazimu kujenga daraja kuvuka ufa ule mkubwa wa dhambi na mauti.

"Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asiangamie, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye" - (Yohana 3:16,17).

Mungu alimtoa Mwanawe, na Yesu alitoa uhai wake kama kafara ya dhambi, akalipa ile adhabu ya mauti yeye mwenyewe. Maisha yake, kifo chake, na ufufuo wake vikafanya uwezekano uwepo wa kuwasamehe na kuwaokoa wenye dhambi bila ya kuihafifisha dhambi, kisha akayaonyesha yale malimwengu tabia halisi ya Kristo na Shetani. Daraja lile lililojengwa kwa mwili wa Kristo ulivunjika na kutoka na damu nyingi linawavuta watu na kuwarudisha nyuma kutoka katika mtego wa dhambi. Upendo unavuka ng'ambo ya ufa huo mkubwa, na kuwawezesha kuvuka ng'ambo na kuingia katika uzima wa milele wale wote wanaoiweka imani yao ndani ya Kristo kama Bwana na Mwokozi wao.

3. Mambo Muhimu Saba Ya Kweli Upaswayo Kuyafahamu Kumhusu Yesu

Mambo hayo saba ya kweli si ya kweli kwa mtu mwingine awaye yote aliyepata kuishi hapa:

(1) Yesu Alitoka Mbinguni. Na Kuja Hapa Duniani Je, Yesu alidai kwamba alikuwako kwa muda gani?
"Kabla Ibrahimu hajazaliwa ulimwengu huu, na kusema: "Mimi Niko!" Mimi nimekuwako siku zote. Ingawa Yesu alizaliwa na mama wa kibinadamu.

Akina Dwight L. Moody, Billy Graham wa karne ile ya kumi na tisa, siku moja walisema hivi juu ya kufanyika mwili kwa Yesu, "Kungekuwa ni kujitolea mhanga kukubwa kwa upande wa Yesu kuja hapa na kubembelezwa katika kitanda kidogo cha fedha cha watoto, kulelewa na malaika, na kulishwa kwa kijiko cha dhahabu. Lakini yule Muumbaji wa mbingu na nchi alikuja hapa na kutwaa mwili wa kibinadamu, na kuzaliwa na wazazi maskini katika zizi la ng'ombe katika mazingira yale mabaya kabisa."

Malaika yule alimwambia Yusufu maneno haya wakati ule wa kuzaliwa kwake Yesu:
"Naye [Mariamu] atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana YEYE ATAWAOKOA WATU WAKE KUTOKA KATIKA DHAMBI ZAO" - (Mathayo 1:21).

Yesu, Muumbaji wa ulimwengu (Yohana 1:1-3,14), kwa hiari yake alitaka kuja katika dhambi na mauti.

(2) Yesu Aliishi Maisha Yasiyo na Dhambi
"Yesu, Mwana wa Mungu,... amejaribiwa kwa kila njia sawasawa na sisi - lakini bila kufanya dhambi" (Waebrania 4:14,15).
Mungu alifanya mengi kuliko kule kusema nasi ili kututaka tutoke katika maisha ya dhambi na kuingia katika maisha yale yanayoridhisha. Kwa kuishi kwake hapa kama mwanadamu, Yesu aliyafanya maisha yake yale yasiyo na dhambi kuwa ya kuvutia sana kuliko hubiri lo lote lile ambavyo lingeweza kufanya.

Shetani, adui yake Kristo alipanga mipango yake mibaya katika kipindi chote cha maisha ya Yesu aliyoishi hapa duniani ili kumshawishi atende dhambi.l kule nyikani Shetani alianzisha mashambulio yake makali mno dhidi ya unyofu wake (Mathayo 4:1-11). Kule Gethsemane kabla ya kusulibiwa kwake, shinikizo la majaribu lilifikia kiwango chake kikubwa kama kile, Yesu alitoa jasho la damu (Luka 22:44).

Lakini Kristo alisimama imara dhidi ya kila kitu alichomtupia Shetani - "lakini bila kufanya dhambi." Kwa kuwa Yesu aliyapitia matatizo yote ya wanadamu na majaribu yao, anaelewa jitihada zetu tunazofanya. Yeye anaweza "kutuhurumia katika udhaifu wetu" (Waebrania 4:15).

Kwa nini ilikuwa ni lazima kwa Yesu kuishi maisha yasiyo na dhambi?
"Mungu alimfanya Yesu, aliyekuwa hana dhambi, kuwa dhambi kwa ajili yetu; na badala ya maisha yetu ya dhambi, Yesu anatupa sisi maisha yake yasiyo na dhambi, ili tuweze kuwa bila dhmbi ndani yake" (2 Wakorintho 5:21, limefafanuliwa).

Yesu aliyashinda majaribu na kuishi maisha yasiyo na dhambi ili atupe sisi hayo kwa kubadilishana na maisha yetu ya dhambi ya zamani.

(3) Yesu Alikufa Kuiondoa Dhambi
Je, ni watu wangapi waliofanya dhambi?
"Kwa sababu WOTE wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu." - Warumi 3:23.

Je, adhabu ya dhambi ni nin?
"Kwa maana Mshahara wa dhambi ni MAUTI; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu" - (Warumi 6:23).

Kwa nini Yesu alikufa?
"Tazama, Mwana-Kondoo wa Mungu, AICHUKUAYE DHAMBI ya ulimwengu!" (Yohana 1:29).
Sisi sote tumefanya dhambi, tena tunakabiliwa na mauti ya milele, lakini

Yesu alikufa badala yetu. Akafanywa kuwa "dhambi kwa ajili yetu." Yeye alilipa hiyo adhabu ya mauti kwa niaba yetu. Kifo chake ni zawadi (karama), na hiyo "KARAMA [ZAWADI] ya Mungu ni UZIMA WA MILELE katika Kristo Yesu Bwana wetu" (Warumi 6:23).

Yesu aliyatoa maisha yake makamilifu, ya haki, kama zawadi yake ya upendo kwetu. Upendo kama ule unapita karibu ufahamu wote wa wanadamu. Na kwa sababu ya kifo chake sisi" tu[na] AMANI kwa Mungu" (Warumi 5:1).

(4) Yesu Alifufuka Kutoka kwa Wafu
Kifo cha Yesu pale msalabani hakikuwa mwisho wa kisa chake cha ajabu. Naam, yeye asingeendelea kuwa mfu wakati huo huo kuwa Mwokozi wetu.
"Na kama Kristo hakufufuka, basi, imani yenu ni bure; mngalimo katika dhambi zenu. Na hapo wao nao waliolala katika Kristo wamepotea" - (1 Wakorintho 15:17,18).

Muhammad na Budha wameupa ulimwengu huu baadhi ya zile kweli kuu za kifalsafa. Wameyaongoza maisha ya mamilioni ya watu, lakini hawana uwezo wa Mungu wa kuwapa uzima kwa maana wao bado wanaendelea kubaki katika makaburi yao.

Kwa kuwa Yesu alifufuka kutoka kaburini siku ile ya tatu baada ya kifo chake, je, ni ahadi gani awezayo kuitoa kwetu?
"Na kwa sababu mimi ni hai, ninyi nanyi mtakuwa hai" Yohana 14:19.

Yesu yu hai! Kwa kuwa yeye anao uwezo juu ya mauti, anaweza kutuokoa toka mautini na kutupa uzima ule ambao ni tele, tena ni wa milele. Ataishi ndani ya mioyo yetu kama tukimkaribisha. Kristo yule aliyefufuka yupo ili kukidhi mahitaji yetu leo.

"Na tazama mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari" - (Mathayo28:20).

Wanaume na Wanawake ulimwenguni kote wanabadilishana visa vyao juu ya jinsi Kristo alivyowaokoa kutoka katika mazoea yao mabaya sana na hisia nzito sana za moyoni mwao ziwatiazo kiwewe.

Mmojawapo miongoni mwa wanafunzi wetu wa zamani aliandika maneno haya ya shukrani katika mojawapo ya karatasi zake za majibu: "Mimi nilikuwa mlevi sugu. Siku moja nilipokuwa nimelewa, niliiona kadi mferejini ikitangaza kozi yenu ya Biblia. Niliiokota, nikaijaza kupata ujuzi wangu wa kwanza wa Kristo. Muda mfupi baada ya kuchukua kozi hiyo ya Biblia, nilitoa moyo wangu kwa Mungu na kuipoteza hamu niliyokuwa nayo kwa wiski. 2

Yesu alipoyatawala maisha ya mtu huyo, nguvu mpya ilimpa uwezo wa kuyashinda mazoea yake yale mabaya. Kwa vile Kristo ni Mwokozi aliyefufuka, anaweza kuwaokoa wote watakaomjia yeye kuomba msaada wake.

(5) Yesu alipaa Mbinguni
Kabla Yesu hajarudi kwa Baba yake baada ya ufufuo wake (Matendo 1:9), alitoa ahadi hii kwa wafuasi wake:
"Msifadhaike mioyo mwenu. Mwaminini Mungu; niaminini na mimi pia nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi;... Ninakwenda kule KUWAANDALIA NINYI MAHALI. Nami.. nitakuja tena na kuwachukua mpate kuwa pamoja nami.... pale nilipo mimi" - (Yohana 14:1-3).

(6) Yesu Anahudumu Kama Kuhani Mkuu
Daima Yesu anajitahidi sana kutuandalia sisi mahali kule mbinguni.
"Ilimpasa kufananishwa na ndugu zake kwa kila njia, ili apate kuwa KUHANI Mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili apate kufanya upatanisho kwa dhambi za watu wake. Na kwa kuwa mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wale wanojaribiwa" (Waebrania 2:17-18).

Yesu alikuja katika dunia yetu ili "kufanya upatanisho kwa dhambi za watu wake," na kutuokoa sisi kutoka katika janga la kuwa watumwa wa dhambi. Alikufa kutuokoa sisi ili hatimaye apate kukifutilia mbali chanzo cha dhambi, maumivu na mauti kwa kumwangamiza Shetani.

Yesu kama Kuhani wetu Mkuu alifananishwa na ndugu zake kwa kila njia." Na sasa anaonekana daima mbele zake Baba kwa ajili yetu kama mpatanishi wetu. Yesu yule yule aliyewabariki watoto, aliyemrudishia heshima yake mwanamke yule aliyekamatwa akizini, na kumsamehe mwizi yule aliyekuwa anakufa pale msalabani, hivi sasa anaendelea kufanya kazi yake kule mbinguni akituhudumia katika mahitaji yetu, ili "kuwasaidia wale wanaojaribiwa."

(7) Yesu Atarudi Tena
Kabla hajarudi mbinguni, Yesu alitoa ahadi gani?
"Nikienda na kuwaandalia mahali, NITAKUJA TENA na kuwachukua kuwa pamaoja nami ili ninyi pia muweze kuwa pale nilipo mimi (Yohana 14:3).

Yesu anaporudi tena, atatuokoa kutoka katika dhambi, magonjwa, misiba, na mauti, mambo ambayo yanaishambulia sayari hii. Naye atatukaribisha katika dunia mpya iliyojaa furaha ya milele na uzima wa milele.

4. Upendo Usiokoma

Hadithi hii inasimuliwa kuhusu ndoa iliyopangwa katika nchi ya Taiwani kati ya U Long na mwanamke kijana aliyeitwa "Ua la Dhahabu." U Long
alipolifunua shela la bibi arusi wake baada ya sherehe ile, alishtuka na kuchukizwa. Uso wake ulikuwa na makovu ya ndui.

Baada ya pale, U Long alikuwa akishughulika na mke wake kwa nadra sana kadiri ilivyowezekana.l alijaribu kadri alivyoweza kumfurahisha; alifanya kazi za nyumbani kwa bidii sana, akitumainia kwamba mume wake hatimaye angeweza kumkubali. Lakini yeye aliendelea kuwa baridi na kutojali kuonyeshwa kule kote kwa upendo wake [mkewe].

Baada ya miaka kumi na miwili ya ndoa yao ile ya kinafiki, U Long alianza kupoteza uwezo wake wa kuona katika macho yake yote mawili. Daktari akamwambia kwamba angekuwa kipofu kabisa kama asingepandikizwa kioo cha macho. Lakini upasuaji ule ulikuwa wa gharama kubwa, tena palikuwa na orodha ndefu ya watu waliokuwa wakingojea upasuaji huo.

Ua la Dhahabu akaanza kufanya kazi kwa masaa marefu jioni akitengeneza kofia za mikeka ili kujipatia fedha za ziada. Siku moja U Long aliambiwa kwamba kioo cha jicho la mtu mmoja kilikuwa kimepatikana baada ya kutokea ajali. Aliharakisha kwenda hospitalini kufanyiwa upasuaji ule.

Baada ya kupona, yeye kwa shingo upande aliamua kumwona mke wake ili aweze kumshukuru kwa kuzipata fedha zile. Alipokigeuza kichwa cha mkewe kilichoinama chini ili mkewe apate kumtazama, U Long alihema kwa mshangao. Mkewe akamkazia macho yake akiwa na macho yasiyoona, yaliyo tupu, kioo cha macho yale kikiwa kimeondolewa. Akiwa amezidiwa na jazba, akaanguka miguuni pa mkewe na kulia kwa kwikwi. Hapo ndipo yeye kwa mara yake ya kwanza alipolitaja jina la mkewe kwa kunong'ona, akasema: Ua la Dhahabu.

Yesu anatamani sana kuwa na uhusiano na wale ambao kwa muda mrefu sana wamekuwa hawamjali. Anatamani kwamba hatimaye sisi tuweze kunong'ona kwa kulitaja jina lake kuwa yeye ndiye Mwokozi wetu. Alijitoa kwa hiari yake sio tu kwa kutoa kafara ya macho yake, bali mwili wake mzima ili apate kutuonyesha upendo wake usiokwisha. Upendo wake una nguvu nyingi sana kiasi kwamba Kristo "alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi" (1 Timotheo 1:15).

Kafara ile kuu aliyotoa Kristo ilijenga daraja linalopita juu ya kutokujali kwetu, linalofunika mfarakano wetu. Je! hivi wewe umegundua mwenyewe kwamba yeye anataka kukuvuta juu ya ufa huo mkubwa na kukukumbatia mikononi mwake? Je! utaitikia na kuomba ukisema, "Yesu, nakupenda wewe. Asante kwa kafara yako ya ajabu mno. Ingia moyoni mwangu na kuniokoa sasa - uniokoe kabisa, uniokoe kikamilifu, uniokoe milele"?

YESU
ALIKUJA kama Mungu katika mwili wa kibinadamu.
ALIISHI maisha yasiyo na dhmbi kwa niaba yetu.
ALIKUFA kwa ajili ya dhambi zetu.
ALIFUFUKA kutuokoa katika mauti.
ALIPAA kwenda kutuandalia makao yetu kule mbinguni.
ANAHUDUMU kila siku kama Kuhani wetu Mkuu.
ANAKUJA UPESI kutuchukua sisi ili tuwe naye milele.


© 2004 The Voice of Prophecy Radio Broadcast
Los Angeles, California, U.S.A.